Na Lucy Ngowi
MKURUGENZI Mkuu wa Taasisi ya Kimataifa ya Kilimo cha Maeneo ya Tropiki (IITA), Dkt. Simeon Ehui amesema Afrika inapaswa kuongeza uzalishaji wa chakula ili kukidhi ongezeko kubwa la watu huku ikiendelea kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabianchi, uharibifu wa ardhi na hali ngumu za kiuchumi.
Dk. Ehui amesema hayo katika hafla ya kutafakari ushirikiano kati ya IITA na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ambapo amesisitiza kuwa mustakabali wa kilimo barani Afrika hautategemea rasilimali pekee, bali ushirikiano wa karibu kati ya serikali, taasisi za utafiti, sekta binafsi, vijana wabunifu na wakulima.
Amesema katika kipindi cha miaka 12 iliyopita, IITA imewekeza takribani Sh bilioni 410.75 nchini Tanzania, sawa na dola za Marekani milioni 154.57, kwa ajili ya shughuli mbalimbali za maendeleo ya kilimo na utafiti.

Kwa mujibu wa Dkt. Ehui, kati ya fedha hizo Sh. Bilioni 318.88 zimeelekezwa katika shughuli za utafiti, huku sehemu ya fedha hizo ikipelekwa kwa Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Tanzania (TARI) pamoja na vyuo vikuu vya ndani.
Aidha, Sh. Bilioni 53.68 zimetumika kulipa mishahara ya wafanyakazi wazawa na Sh. Bilioni 38.19 kuwekeza katika miundombinu na vifaa.
Amesema taasisi hiyo pia imewekeza katika maendeleo ya rasilimali watu kwa kufadhili wanafunzi 60 wa shahada za uzamivu na wanafunzi 80 wa shahada za uzamili, pamoja na kutoa mafunzo kwa zaidi ya vijana 10,000 na wakulima zaidi ya 11,000.
“Nyuma ya takwimu hizi kuna maisha yaliyobadilika, vijana waliowezeshwa na matumaini mapya kwa jamii za wakulima,” amesema.

Dkt. Ehui ameishukuru Serikali ya Tanzania kwa ushirikiano wake wa muda mrefu na kumpongeza Rais Mstaafu Jakaya Kikwete kwa mchango wake katika kuimarisha uwepo wa IITA nchini tangu mwaka 2013.

