Na Lucy Ngowi
MWANZA: MHAIDROJIOLOJIA kutoka Bodi ya Maji Bonde la Ziwa Victoria (LVBWB), Jackline Jacob, amesema taasisi hiyo inaendelea kufanya tathmini ya wingi na ubora wa maji katika Bonde la Ziwa Victoria kwa lengo la kuhakikisha rasilimali hiyo inalindwa na kutumika kwa uendelevu.
Amesema pamoja na jukumu hilo, bodi hiyo pia inasimamia ugawaji wa maji kupitia utoaji wa vibali pamoja na kulinda na kuhifadhi vyanzo vya maji katika maeneo mbalimbali ya bonde hilo.
Jackline ametoa kauli hiyo wakati akizungumza kwenye maonesho ya Ziwa Victoria yanayoendelea jijini Mwanza.
Aidha, amewahimiza wananchi kuzingatia sheria za uhifadhi wa mazingira kwa kuepuka kufanya shughuli za kibinadamu ndani ya mita 60 kutoka kwenye vyanzo vya maji.
Amefafanua kuwa vyanzo vya maji vinavyopaswa kulindwa ni pamoja na mito, vijito na Ziwa Victoria, ambavyo vina mchango mkubwa katika maisha ya wananchi na shughuli za kiuchumi.

