Na Lucy Lyatuu,Tanga
MWANAFUNZI wa Chuo Kikuu Cha Ardhi (ARU) Vinod Valence amebuni utengenezaji wa vigae vinavyotokana na chupa za plastiki za rangi baada ya kuzirejelesha.
Chupa zinazotumika ni za rangi zinazotumika kuweka vinywaji vya kuongeza nguvu,ambazo soko lake la urejelezaji ni dogo hiku zikiachwa kuchafua mazingira.
Valence amesema hayo wakati akizungumza katika banda la Ardhi katika maadhimisho ya wiki ya Elimu Ujuzi Na Ubunifu 2026 yanayofanyika katika viwanja vya Usagara Tanga.
Kuhusu mchakato wa utengenezaji, chupa za plastiki za rangi huyeyushwa na kupata mchanganyiko unaochanganywa na mchanga wa kawaida.
“Mchanganyiko huo huwekwa kwenye mold mbalimbali kulingana na ukubwa na mahitaji ya mteja, na hatimaye kutengeneza vigae vya ukubwa tofauti,” amesema.
Amesema vigae hivyo vimetengenezwa mahsusi kwa ajili ya kuwekwa kwenye kuta za vyoo, mabafu na jikoni, na si kwa matumizi ya sakafuni kutokana na sehemu yake ya juu kuwa laini.
Ameongeza kuwa, ubunifu huo unalenga pia kutoa bidhaa yenye bei nafuu ambayo inaweza kumudu kutumiwa na wananchi wenye viwango tofauti vya kipato.
Aidha amesema mbali na kutatua changamoto ya taka za plastiki, ubunifu huo unaweza kutoa soko kwa wakusanyaji wa chupa za plastiki, ambao wataweza kukusanya chupa hizo na kuzipeleka kwa ajili ya kuchakatwa na kuzalisha bidhaa mpya.
Kuhusu hatua ya kupata ithibati, Valence amesema kwa sasa wanaendelea na uzalishaji wa vigae hivyo kwa wingi ili kufanya majaribio zaidi, kabla ya kuwasilisha bidhaa hiyo kwa Shirika la Viwango Tanzania (TBS) kwa ajili ya kufanyiwa vipimo na kuthibitishwa kwa matumizi ya sokoni.
“Tayari tumefanya majaribio ya awali kwa kutumia vigae hivyo kwenye kuta za vyoo, mabafu na jikoni, na tumepata maoni kutoka kwa wananchi katika maonyesho mbalimbali tunayoshiriki,” amesema.


