Na Lucy Ngowi
DAR ES SALAAM: CHUO Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), kimetumia teknolojia ya kidijitali katika kukabiliana na tatizo la sumu kuvu.
Profesa kutoka Idara ya Sayansi na Teknolojia za Chakula, chuoni hapo, Lilian Kaale amesema hayo alipozungumza na Mfanyakazi Tanzania.
Amesema kwa kutumia teknolojia hiyo wameangalia zile hali zinazomfanya huyo mdudu ambaye anatoa sumu ambayo ndio sumukuvu na kuidhibiti.
“Teknolojia hii imewekwa sensa ambayo ina sensi joto, mvuke pamoja na unyevunyevu, hizi ni hali tatu kubwa kama hazijafikia kile kiwango cha wadudu kutoa sumu, hawatoi sumu. Kwa hiyo teknolojia ikianza kufikia kile kiwango kwa ajili ya kutoa sumu inakupa taarifa, pia inarudisha zile hali kuzuia wadudu wasizalishe sumu.
“Kwa hiyo ni teknolojia nzuri. tumeshaiweka kwenye ghala mojawapo la kuhifadhia lililopo eneo la Chemba Dodoma na sasa inafanya kazi,” amesema.
Amesema kwa hatua hiyo, wanaangalia ni jinsi gani wanaweza kuishauri serikali na kuandika sera kwa ufupi, kuona jinsi gani ya kuendeleza teknolojia iende kwenye maghala ya kuhifadhi chakula ambayo yako Tanzania.
Amesema tatizo hilo la sumukuvu linashambulia zaidi mahindi na karanga.
“Ukiangalia mahindi kila mtanzania anakula mahindi kwa maana nyingine ni kwamba tukiathirika kwenye mahindi tutapoteza nguvu kazi kubwa ya watanzania maana yake watakufa.
“Watakufa kwa kuwa sumu kuvu inaua inasababisha kansa ya ini na ukiangalia utafiti uliofanyika 2018 unaonyesha asilimia 8.2 ya vifo vinavyopatikana duniani vinatokana na kansa ya ini. Na sumu kuvu inachangia kwa kiasi kikubwa kusababisha kansa ya ini,” amesema.
Profesa huyo amesema tatizo lililojitokeza Chemba mwaka 2015 na kuua baadhi ya watu ndilo lililomvutia kufanya utafiti huo.
Kwamba baada ya vile vifo vilivyotokea Chemba, serikali ilipeleka sampo Marekani pamoja na Belgium kupima kuona tatizo lilikuwa ni nini ikagundulika kuwa ni sumu kuvu hapo utafiti ukaanza kwa kasi nchini Tanzania.
Amesema hivyo nao chuo kikuu hicho wakaona wafanye utafiti huo kwa kutumia teknolojia hiyo ya kidijitali.