Na Lucy Ngowi
DAR ES SALAAM: WADUDU aina ya senene wameongezewa thamani kwa kufanyiwa utafiti wa kutolewa mafuta ambayo hutumika kama dawa, kisha mabaki yake husagwa kwa ajili ya kupikia vyakula mbalimbali vya kuokWa ikiwepo keki.
Profesa Kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Idara ya Sayansi na Teknolojia za Chakula, Lilian Kaale amesema hayo katika Maadhimisho ya 10 ya Wiki ya Utafiti na Ubunifu inayohitimishwa leo Juni 11, 2025 chuoni hapo alipokuwa akizungumza na Mwandishi wa Mfanyakazi Tanzania.
Amesema, “Sasa hivi ukila senene wakiwa bado hawajaongezewa thamani unakuta wana mafuta mengi sana na tukaona kwa nini tusitoe kwanza yale mafuta,
“Na tulichofanya hapa tumetoa mafuta, na hayo mafuta tumeyafanyia utafiti tukaona yana virutubisho vizuri sana kwa kifupi mafuta hayo yanatumika kama dawa sio mafuta ya kawaida,”.
Amesema mafuta hayo yana virutubisho vikubwa vitatu ambavyo ni Omega 3, Omega 6 na Omega 9, hivyo mtumiaji wa mafuta hayo hutumia kama dawa kwa kuchanganya kiasi kidogo na chakula kinapokuwa kimeiva tayari.
Virutubisho hivyo vinajenga mwili na vinaweka chembe chembe za mwili kuwa imara.
“Baada ya kutoa hayo mafuta yale mabaki ya senene yaliyobakia yakatengenezwa unga, huo unga mtu akitaka kutumia anaweza kuchanganya na unga wa mahindi akatengeneza uji au unachukua, unachanganya na unga wa ngano unatengeneza mikate, biskuti, na bidhaa nyingine. Kwa hiyo mtu akila anakula vyakula vyenye virutubisho vya kutosha.
“Kwa hiyo kwa haraka utaona kilo moja ya senene inaweza ikanufaisha mkulima, jamii au mtu mmoja mmoja kwa kiasi kikubwa kwa kuwa chupa ndogo ya ujazo 200 mafuta yake ni sh 20,000 kwa sababu ya hivyo virutubisho vilivyopo,” amesema.
Amesema wamebuni mradi huo wa wadudu hao wanaopatikana mkoani Kagera kwa kuwa hakuna mtu aliyeongeza thamani kwenye hao senene.
Amesema kama watafiti na wabunifu lengo lao ni kutafuta majawabu ya matatizo katika jamii, na wanavyotafuta matatizo hayo na kuyathibitisha kinachofuata ni kutafuta wawekezaji wanaoweza kuichukua hiyo teknolojia ili wazalishe kwa wingi na kuuza kwenye jamii.