Na Lucy Ngowi
“WENGI wanapokosa kipato wanapata shida, ili kuwe na mwendelezo wa kipato mfuko upo kwa ajili ya kuchukua nafasi hiyo,”.
Mwendeshaji Mkuu wa Mfuko wa Hifadhi ya Jamii wa Hiari(WRF), Muchunguzi Kabonaki amesema hayo wakati akizungumza na Mwandishi wa MFANYAKAZI.
Kabonaki amesema lengo la kuanzishwa kwa mfuko huo ni kuhakikisha watanzania wengi wanapata huduma ya hifadhi ya jamii.
Ameshauri watanzania kutumia fursa hiyo ya kujiwekea hifadhi kwa siku ambazo hawatakuwa na nguvu ya kuzalisha kipato.
Pia amesema kanuni ya mfuko huo ni kila mwanachama kuchangia angalau shilingi 10,000 kwa mwezi kupitia kwa mwajiri ama mwanachama mwenyewe kulipa mchango wake.
Kwa upande mwingine amesema mfuko huo upo kwenye mazungumzo na kampuni za simu ili wanachama walipe kupitia mitandao ya simu.
Vile vile amesema wanatarajia kuutanganza mfuko huo kuanzia Oktoba mwaka huu, kwa kuzungumza na waajiri, kuendesha semina na Maofisa Utumishi pamoja na kutumia vyombo vya habari.
Mfuko huo umeanzishwa mwaka jana kwa lengo la kutoa hifadhi ya jamii ya nyongeza kwa wanachama wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania ( TUCTA), na Sekta Isiyo Rasmi.