Asema uanachama GGGI utafungua fursa za teknolojia, fedha za miradi ya tabianchi
Na Lucy Ngowi
Dodoma: TANZANIA inahitaji kuwekeza katika teknolojia za kisasa zitakazowezesha Serikali kufuatilia uharibifu wa mazingira nchini kote na kufanya tathmini sahihi ya hewa ukaa (carbon), Profesa Pius Yanda amesema.
Akichangia Azimio la Bunge kuhusu kuridhia uanzishwaji wa Taasisi ya Kimataifa ya Ukuaji wa Kijani (Global Green Growth Institute-GGGI), Profesa Yanda amesema uanachama wa Tanzania katika taasisi hiyo unaweza kuongeza uwezo wa nchi kupata teknolojia, utaalamu na fursa za fedha kwa ajili ya miradi ya mazingira na mabadiliko ya tabianchi.
GGGI ni taasisi ya kimataifa ya kiserikali inayolenga kusaidia nchi zinazoendelea na zinazoibukia kukuza uchumi kwa namna inayolinda mazingira, kupunguza uzalishaji wa hewa chafu na kuongeza ustahimilivu dhidi ya mabadiliko ya tabianchi.
Pia husaidia nchi kuandaa miradi ya kijani na kuchochea upatikanaji wa uwekezaji na fedha kwa miradi hiyo.
Profesa Yanda amesema Tanzania, kama zilivyo nchi nyingine zinazoendelea, inakabiliwa na athari za mazingira na mabadiliko ya tabianchi, hivyo inahitaji rasilimali, teknolojia na kujengewa uwezo ili kukabiliana na changamoto hizo.
“Katika eneo la tathmini ya hewa ukaa (carbon), tunahitaji teknolojia zaidi,” amesema Profesa Yanda.
Amesema mahitaji hayo yanakuwa muhimu zaidi kutokana na kuongezeka kwa majukumu ya kusimamia mazingira, akisisitiza umuhimu wa Tanzania kuwa na mfumo wa kiteknolojia unaoweza kufuatilia hali ya mazingira katika maeneo mbalimbali ya nchi kwa ufanisi.
“Tunahitaji kufikia hatua ya kuwa na teknolojia inayoweza kufuatilia uharibifu wa mazingira katika maeneo mbalimbali ya nchi kwa ufanisi. Haya yote yanahitaji ushirikiano na taasisi kubwa kama GGGI,” amesema.
Profesa Yanda amesema Serikali tayari imekuwa ikishirikiana na taasisi za kimataifa, zikiwemo UNEP na UNDP, ambazo zimekuwa zikisaidia katika maeneo ya teknolojia, kujenga uwezo na kuwezesha upatikanaji wa fedha kwa ajili ya miradi ya mazingira na mabadiliko ya tabianchi.
Amesema taasisi hizo huwezesha nchi kupata fedha kupitia mifuko ya kimataifa ya mabadiliko ya tabianchi, ikiwemo GEF na GCF, huku akieleza kuwa GGGI inaweza kuwa taasisi ya ziada itakayosaidia Tanzania kufikia malengo yake ya maendeleo ya kijani.
Profesa Yanda amesema hatua hiyo inaendana na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, ambayo imeweka mazingira na mabadiliko ya tabianchi miongoni mwa maeneo muhimu ya maendeleo ya Tanzania.
Amesema Tanzania ina kila sababu ya kuimarisha ushirikiano na GGGI na kutumia fursa zitakazopatikana, lakini akasisitiza umuhimu wa Serikali kuandaa mapema mawazo na mapendekezo ya miradi yenye ubora ili iweze kunufaika na fursa za fedha na teknolojia.
“Tuna kila sababu sasa ya kuhakikisha kwamba na sisi tunakuwa wanachama ili tuweze kunufaika na taasisi hiyo,” alisema.
Taarifa ya GGGI inaonyesha Tanzania ipo katika hatua ya mchakato wa kujiunga na taasisi hiyo, pamoja na nchi nyingine kadhaa.
Profesa Yanda amehitimisha kwa kuunga mkono Azimio hilo.


