Yataka Mapengo YA Sheria Yaliyopo Yabainishwe
Na Lucy Ngowi
SERIKALI imeagiza kufanyika kwa utafiti wa kina kuhusu umuhimu wa kutungwa kwa Sheria mahsusi ya Biashara Mtandao (E-Commerce Law), ikiwa ni hatua ya kukabiliana na changamoto za kisheria zinazojitokeza kutokana na kasi ya ukuaji wa uchumi wa kidijitali nchini.
Waziri wa Katiba na Sheria, Dkt. Juma Homera, ametoa agizo hilo katika kikao na Katibu Mtendaji wa Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania, George Mandepo, kilichojadili maboresho ya sheria yanayolenga kuunga mkono utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Katika kikao hicho, viongozi hao walitathmini namna mabadiliko ya teknolojia na ongezeko la matumizi ya majukwaa ya kidijitali katika kufanya biashara yanavyohitaji mfumo wa sheria unaokwenda sambamba na mazingira hayo.
Kwa mujibu wa maelekezo hayo, utafiti utapitia sheria zilizopo ili kubaini mapengo na changamoto za kisheria zinazohusiana na biashara mtandao, pamoja na kufanya ulinganisho na mifumo ya sheria inayotumika katika nchi nyingine.
Miongoni mwa maeneo yatakayochunguzwa ni mikataba ya kielektroniki, ulinzi wa watumiaji, uendeshaji wa majukwaa ya kidijitali, malipo ya kielektroniki na ulinzi wa taarifa binafsi.
Pia, utafiti huo utazingatia usalama wa miamala ya kielektroniki, haki miliki, masuala ya kodi, ushindani na namna ya kutatua migogoro inayotokana na biashara zinazofanyika mtandaoni.
Biashara mtandao imeendelea kuwa sehemu muhimu ya shughuli za kiuchumi, ikirahisisha uuzaji wa bidhaa na huduma kupitia teknolojia za kidijitali katika sekta mbalimbali, ikiwemo kilimo.
Waziri Homera ameitaka Tume ya Kurekebisha Sheria kuanzisha utafiti huo na kuandaa mapendekezo yatakayowezesha Serikali kuamua iwapo kuna haja ya kutungwa kwa Sheria mahsusi ya Biashara Mtandao au kufanyiwa maboresho sheria zilizopo.
Serikali inaona hatua hiyo kuwa muhimu katika kujenga mazingira salama na rafiki kwa wafanyabiashara na watumiaji wa huduma za kidijitali, huku ikichochea ubunifu, ushindani na uwekezaji katika uchumi wa kidijitali.
Aidha, matokeo ya utafiti yanatarajiwa kusaidia Tanzania kutumia kikamilifu fursa zinazotokana na uchumi wa kidijitali na kuimarisha ulinzi wa maslahi ya wafanyabiashara na watumiaji.


