Na Lucy Ngowi
DODOMA: WAKATI ongezeko la shughuli za Serikali, biashara na ujenzi likiendelea kuongeza msongamano wa magari Dodoma, Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) umeanza kupanua mtandao wa barabara ili kufungua njia mbadala za usafiri na kurahisisha uunganishaji wa maeneo mbalimbali ya mji.
Mhandisi wa TARURA Mkoa wa Dodoma, Revocatus Daniel Nsubile, amesema hayo katika maonesho ya nane nane yaliyomalizika na kuongeza, maboresho hayo yanalenga kuimarisha mawasiliano kati ya Dodoma mjini na maeneo muhimu, ikiwamo Chamwino ambako kuna Mji wa Serikali na taasisi mbalimbali.
Amesema uboreshaji wa barabara hizo utawapa wananchi njia mbadala za usafiri na kusaidia kupunguza utegemezi wa barabara zinazotumika kwa wingi, hatua inayotarajiwa kurahisisha usafiri na shughuli za kiuchumi.
“Tunapoendelea kuboresha barabara hizi, tunalenga kuwasaidia wananchi kufika maeneo yao kwa urahisi na pia kupunguza msongamano katika barabara zinazotumika kwa wingi,” amesema.
Nsubile amesema TARURA Mkoa wa Dodoma unasimamia mtandao wa barabara katika wilaya saba za mkoa huo, huku ujenzi, ukarabati na matengenezo ukiendelea.
Amesema kwa mwaka wa fedha 2026/27, TARURA imeanza mchakato wa utekelezaji wa miradi mipya, ikiwamo uboreshaji wa barabara zinazolenga kuongeza ufanisi wa usafiri.
Amesema barabara bora pia zitasaidia wakulima kusafirisha mazao kutoka maeneo ya uzalishaji kwenda masokoni kwa urahisi.
Aidha, amewataka wananchi kulinda miundombinu ya barabara, ikiwamo taa na alama, na kutoa taarifa za wizi au uharibifu kwa viongozi na vyombo vya ulinzi na usalama.

