Na Lucy Ngowi
DODOMA: RAIS Dkt. Samia Suluhu Hassan amesema Serikali imeamua kutumia Vyama vya Ushirika kama nguzo muhimu katika usimamizi na utoaji wa huduma za zana za kilimo kwa wakulima nchini, akieleza kuwa taasisi hizo ziko karibu na wakulima na zinaelewa mahitaji yao.
Rais Samia amesema uamuzi huo unalenga kuhakikisha matrekta na zana nyingine za kilimo zitakazokabidhiwa kwa Vyama vya Ushirika zinatumika ipasavyo kuongeza tija, uzalishaji na kipato cha wakulima katika maeneo yao.
Akizungumza hayo wakati wa hafla ya kukabidhi vitendea kazi kwa Wakala wa Taifa wa Huduma za Ugani (NAESA) na Vyama vya Ushirika, Rais Samia amesema Serikali awali ilikuwa na mpango wa kuanzisha vituo vya zana za kilimo katika Kanda mbalimbali nchini.

Hata hivyo, amesema baada ya kutafakari namna bora ya kuwafikishia wakulima huduma hizo, Serikali imeona Vyama vya Ushirika vina nafasi kubwa zaidi kutokana na kuwa karibu na wakulima.
“Sasa tunaanza na nyie, nitakabidhi matrekta yaliyopo hapa yaende yakafanye kazi. Tutaendelea kununua hadi tueneze kama tulivyoahidi,” amesema.
Amesema Vyama vya Ushirika vitakuwa na jukumu la kusimamia matrekta hayo na kuhakikisha yanawafikia wakulima wanaohitaji huduma za zana za kilimo kwa wakati.
“Tumewakabidhi matrekta haya na zana tutakazonunua kwa Vyama vya Ushirika ili wao wawasimamie wakulima wao,” amesema.
Rais Samia amesisitiza kuwa matrekta na zana hizo hazipaswi kutumika kinyume na malengo yaliyokusudiwa, bali ziendelee kuwa sehemu ya juhudi za Serikali kuwawezesha wakulima kuongeza uzalishaji.
Amesema Serikali itaendelea kununua na kukabidhi matrekta pamoja na zana nyingine za kilimo kwa Vyama vya Ushirika katika Kanda mbalimbali, hatua inayolenga kupunguza changamoto ya upatikanaji wa zana na kuongeza tija katika kilimo.
Kwa mujibu wa Rais Samia, mfumo huo utaiwezesha Serikali kuwafikia wakulima kwa ufanisi zaidi kupitia Vyama vya Ushirika, huku vyama hivyo vikitakiwa kuhakikisha vifaa vinavyokabidhiwa vinawanufaisha wakulima na kuchochea maendeleo ya kilimo katika maeneo yao.


