Na Lucy Lyatuu,Dodoma
MAMLAKA Ya Udhibiti Mkondo wa Juu wa Petroli (PURA), inahamasisha vijana kujenga ujuzi unaohitajika katika sekta ya mafuta na gesi, na kuvitaka vyuo mbalimbali vikuu kujumuisha masomo yanayohusiana na sekta hiyo katika mitaala yao.
Mkurugenzi Mkuu wa PURA, Charles Sangweni amesema hayo wakati akizungumza na waandishi wa habari katika banda la PURA katika maonesho ya kilimo Nanenane jijini Dodoma.
Amesema ushiriki wa mamlaka hiyo katika Maonesho ya Nane Nane unalenga kuwaelimisha wananchi kuhusu shughuli za mkondo wa juu wa sekta ya mafuta na gesi pamoja na fursa zinazopatikana katika sekta hiyo.
Amesema Serikali inaendelea kushirikisha taasisi za elimu ya ufundi, ikiwemo VETA, ili kuongeza idadi ya wataalamu wenye ujuzi wanaoweza kushiriki katika shughuli za sekta hiyo.
Sangweni amesema mamlaka hiyo pia inahakikisha wazawa wanashiriki kikamilifu kupitia ajira, utoaji wa huduma na usambazaji wa bidhaa katika shughuli za mafuta na gesi.
Hata hivyo, amesema bado kuna changamoto ya upatikanaji wa wataalamu wenye ujuzi wa juu na baadhi ya bidhaa zinazohitajika na wawekezaji, hali inayosababisha kutegemea wataalamu na bidhaa kutoka nje ya nchi.
Amesema Tanzania ina maeneo yenye viashiria vya uwepo wa mafuta na gesi asilia, huku tafiti za kijiolojia na tafsiri za data zilizofanyika hadi sasa zikifunika takribani asilimia 30 ya maeneo yanayoaminika kuwa na rasilimali hizo.
Amesema PURA, iliyoanzishwa kwa mujibu wa Sheria ya Petroli ya mwaka 2015, ina jukumu la kusimamia na kudhibiti shughuli za mkondo wa juu wa petroli, kutoa ushauri kwa Serikali, kuhakikisha sheria na taratibu zinafuatwa, kuongeza manufaa ya rasilimali kwa Taifa, pamoja na kusimamia usalama na ulinzi wa mazingira.
Amesema PURA inaendelea kutekeleza majukumu yake kwa kuzingatia Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050, ikiwemo kusimamia miradi ya kimkakati katika sekta ya gesi. Miongoni mwa miradi hiyo ni mpango wa kuchakata gesi asilia na kuibadilisha kuwa kimiminika (LNG), unaotarajiwa kujengwa mkoani Lindi kwa lengo la kuiwezesha Tanzania kushiriki zaidi katika soko la kimataifa la gesi.

