Na Lucy Lyatuu,Dodoma
HALMASHAURI Ya Jiji La Dodoma limewataka wakulima na wananchi kutumia Maonesho ya Nane Nane kujifunza teknolojia za kisasa za uzalishaji wa mazao, ikiwemo kilimo cha mbogamboga na maua, ili kuongeza tija na kujenga fursa za kiuchumi kupitia kilimo.
Akizungumza katika kitalu cha mbogamboga,maua na miti ya matunda katika viwanja vya Maonesho ya Nane Nane, Mtaalamu wa Kilimo anayesimamia Sekta ya Mazao katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Agnes Loiso amesema maonesho hayo ni fursa muhimu kwa wakulima kupata elimu ya vitendo kuhusu uzalishaji wa mazao mbalimbali kwa kutumia teknolojia zinazoweza kuongeza tija.


Amesema katika maonesho hayo, wakulima watafundishwa namna ya kuzalisha mboga za aina mbalimbali pamoja na maua, ambayo yameanza kuwa fursa ya biashara na ujasiriamali kwa wananchi.
“Wakulima wanashauriwa kujihusisha na uzalishaji wa maua kama wajasiriamali kwa sababu nao ni biashara inayoweza kuwa chanzo cha kipato,” amesema.
Amesema Halmashauri ya Jiji la Dodoma pia imefanya majaribio ya baadhi ya mazao, ikiwemo mapera na zabibu, ambayo yameonyesha matokeo mazuri na baadhi yako tayari yameanza kuzaa matunda.


Ameongeza kuwa changamoto zilizojitokeza katika uzalishaji wa baadhi ya mazao zilitokana zaidi na mabadiliko ya hali ya hewa, hususan kwa mazao yanayohitaji baridi kali.
“Hali ya hewa ilitusumbua kidogo kwenye baadhi ya mazao ambayo yanahitaji baridi kali, lakini mwisho wa siku yalitoa maua japokuwa hayakuwa makubwa sana,” amesema.
Aidha amewataka wananchi wenye maeneo madogo au ambao wamejenga nyumba na kuweka matofali chini kutokata tamaa ya kujihusisha na kilimo, akisema teknolojia za bustani za nyumbani zinaweza kuwa suluhisho.
Amesema wananchi wanaweza kujifunza namna ya kuzalisha mbogamboga katika maeneo madogo yaliyopo nyumbani na kupata chakula kwa matumizi ya familia pamoja na ziada ya kuuza.


“Unaweza ukazalisha mboga hata kama huna eneo kubwa la kilimo. Waje wajifunze, wajionee wenyewe na waende wakajaribishe majumbani mwao,” amesema.
Kuhusu dhana kuwa Jiji la Dodoma ni kame nanhalifainkwa kilimo amesema eneo hilo lina uwezo wa kuzalisha mazao mbalimbali kutokana na uwepo wa maji chini ya ardhi.
Amesema katika maeneo mbalimbali ya Dodoma, maji yanaweza kupatikana kwa kuchimba visima kwa kina kifupi, jambo linalowapa wakulima fursa ya kufanya kilimo cha umwagiliaji.
“Dodoma siyo kame kama wananchi wanavyosema. Maji yapo mengi chini ya ardhi na katika baadhi ya maeneo ukichimba mita chache unakutana na maji,” amesema.
Amesema hali hiyo imewezesha majaribio ya mazao mbalimbali kufanyika na kuonyesha matokeo mazuri, ikiwemo ngano, karoti, vitunguu viazi, mbaazi,uwele na ufuta huku akisisitiza kuwa wakulima wanaweza kutumia fursa hiyo kuongeza uzalishaji na kipato.


Ameeleza kuwa Maonesho ya Nane Nane yanatoa nafasi kwa wananchi kuona kwa vitendo teknolojia na mbinu mbalimbali za kilimo, hivyo kuwataka wakulima kutoka maeneo mbalimbali kufika na kujifunza namna bora ya kuongeza tija katika uzalishaji.

