Na Lucy Lyatuu,Dodoma
WAKALA wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA) umesema inatumia maonesho ya nanenane kutoa elimu kuhusu mfumo mpya wa usajili ulioboreshwa, ambao umefanyiwa maboresho ili kurahisisha upatikanaji wa huduma na kupunguza changamoto ambazo baadhi ya wafanyabiashara walikuwa wakikumbana nazo.
Wakala hio umesema kupitia mfumo huo mpya, baadhi ya huduma zinaweza kufanyika kwa njia ya mtandao bila mhusika kulazimika kufika moja kwa moja katika ofisi za BRELA.
Ofisa Usajili kutoka BRELA, Yusuf Mwasakafika, amesema hayo wakagi akizungumza katika banda hilo na kuwataka wafanyabiashara, wakulima na wananchi kutumia fursa ya Maonesho hayo kupata huduma mbalimbali za usajili na leseni, huku ukitoa elimu kuhusu maboresho ya mfumo wake mpya wa usajili.
Amesema BRELA imesogeza huduma zake katika Maonesho ya Nane Nane yanayofanyika katika Viwanja vya Nane Nane, Dodoma, kuanzia Agosti Mosi hadi Agosti Nane, mwaka 2026, ili kuwawezesha wananchi kupata huduma ambazo kwa kawaida huzipata katika ofisi za taasisi hiyo.
Amesema wananchi wanaweza kupata huduma mbalimbali ikiwemo usajili wa majina ya biashara, usajili wa kampuni, utoaji wa leseni za biashara kundi A pamoja na huduma zinazohusiana na usajili wa alama za biashara na viwanda.
Amesema uwepo wa BRELA katika maonesho hayo unalenga pia kuwahamasisha wakulima wanaofanya kilimo cha kibiashara kurasimisha shughuli zao ili waweze kujiamini zaidi katika kufanya biashara na kufikia masoko na wadau mbalimbali.
Amewahamasisha wafanyabiashara na wananchi kwa ujumla wanaofanya shughuli mbalimbali za kilimo kufika katika banda hilo kupata huduma ambazo wangeweza kuzitafuta wakiwa ofisini, lakini sasa wanaweza kuzipata hapo.
Amesema miongoni mwa maboresho yaliyofanyika ni kuwezesha uwasilishaji wa nyaraka mbalimbali kwa njia ya mfumo, ikiwemo nyaraka zinazohusiana na madeni yanayohitaji kuwasilishwa katika usajili.
“Kwa kutumia mfumo huu sasa tumeweza kuboresha huduma kiasi kwamba mtu anaweza kuwasilisha nyaraka akiwa nyumbani kwake au benki, bila kulazimika kufika BRELA,” amesema.
Amesema pia mfumo huo umeboresha upatikanaji wa taarifa za kampuni kwa wananchi wanaohitaji taarifa hizo, huku ukiongeza uwazi kuhusu taarifa za kampuni kulingana na huduma inayohitajika.
Mwasakafika amesema maboresho mengine ni katika suala la usalama wa taarifa za kampuni, ambapo wanahisa wanapata taarifa pale kampuni inapofanya mabadiliko yanayohusiana na kampuni yao.
Hata hivyo, amewataka wananchi wanaotaka kutumia mfumo huo kuhakikisha wanakuwa na namba ya kitambulisho cha Taifa (NIDA), namba ya simu inayotumika pamoja na anuani sahihi ya barua pepe, ambazo ni muhimu katika kupata huduma kupitia mfumo.
BRELA inasimamia utekelezaji wa sheria mbalimbali zinazohusu usajili na urasimishaji wa biashara nchini, ikiwemo usajili wa kampuni, majina ya biashara, alama za biashara na huduma za leseni zinazohusika na taasisi hiyo.
Katika Maonesho ya Nane Nane, BRELA inapatikana katika banda la Makamu wa Rais na Waziri Mkuu pamoja na banda la Wizara ya Viwanda na Biashara, ikiwa na lengo la kuwafikia wananchi na kuwapatia huduma pamoja na elimu kuhusu urasimishaji wa shughuli zao za biashara

