Na Lucy Ngowi
DODOMA: MAMLAKA ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA) imewahimiza vijana, wanawake, wazee na watu wenye ulemavu kujitokeza kwa wingi kujisajili katika mfumo wa ununuzi wa umma ili kunufaika na fursa za zabuni za serikali.
Wito huo umetolewa na Mkurugenzi Mkuu wa PPRA, Dennis Simba, wakati wa Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yaliyomalizika jijini Dodoma, ambapo amesema Serikali imeweka mazingira rafiki ya ushiriki wa wananchi katika shughuli za kiuchumi kupitia Sheria ya Ununuzi wa Umma ya mwaka 2023 na kanuni zake za mwaka 2024.
Simba amesema sheria hiyo, ambayo aliitaja kuwa ya kizalendo, imeelekeza taasisi zote za umma kutenga asilimia 30 ya bajeti zao za ununuzi kwa ajili ya makundi maalum ya vijana, wanawake, wazee na watu wenye ulemavu.
Amesema hatua hiyo inalenga kuhakikisha wananchi wengi zaidi wananufaika na matumizi makubwa ya fedha za umma kupitia fursa za zabuni zinazotolewa na serikali.
“Tunamshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa maelekezo yake yaliyowezesha kupitishwa kwa sheria hii ambayo imefungua milango ya ushiriki mpana wa wananchi katika biashara na serikali.
Hii ni fursa muhimu kwa Watanzania,” amesema Simba.
Amebainisha kuwa hadi sasa zaidi ya vikundi 8,700 vimesajiliwa katika mfumo wa kitaifa wa ununuzi wa umma kielektroniki (NeST), huku thamani ya zabuni zilizotolewa kwa makundi maalum ikifikia takribani Sh bilioni 50 na mikataba iliyosainiwa ikizidi Sh bilioni 45.
Aidha, amesema PPRA kwa kushirikiana na Wizara ya Fedha na Ofisi ya Rais imeendelea kutoa elimu nchini kote ili kuhakikisha wananchi wanaelewa na kutumia fursa hizo ipasavyo.
Amewataka pia wanahabari kuendelea kuelimisha umma kuhusu umuhimu wa kujisajili katika mfumo huo, akisisitiza kuwa hakuna ubaguzi katika upatikanaji wa zabuni za serikali.
Simba amehitimisha kwa kuwataka wadau wa sekta binafsi kushiriki Kongamano la Ununuzi wa Umma litakalofanyika Arusha mwishoni mwa Julai, likilenga kujadili mafanikio, changamoto na maboresho ya mfumo huo.

