Na Lucy Ngowi
DODOMA: WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Ridhiwani Kikwete, ameipongeza Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) kwa juhudi zake katika kusimamia sekta za nishati na maji pamoja na kuwahudumia wananchi kwa ufanisi.
Ridhiwani ametoa pongezi hizo leo Juni 17, 2026, alipotembelea banda la EWURA katika Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea katika viwanja vya Chinangali Park jijini Dodoma.
Akizungumza baada ya kupata maelezo kuhusu shughuli zinazotekelezwa na mamlaka hiyo, Ridhiwani amesema ameridhishwa na namna EWURA inavyotekeleza majukumu yake na kusogeza huduma karibu zaidi na wananchi.

“Hongereni sana kwa kazi kubwa mnayoifanya,” amesema Waziri huyo.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Utawala na Usimamizi wa Rasilimali Watu wa EWURA, Hawa Mniga, amesema mamlaka hiyo imejitokeza katika maadhimisho hayo ili kutoa elimu kwa umma kuhusu huduma zake pamoja na kupokea na kushughulikia kero mbalimbali zinazowakabili wananchi katika sekta za nishati na maji.
Ameeleza kuwa wananchi wanaotembelea banda la EWURA wanapata fursa ya kufahamu majukumu ya mamlaka hiyo, kuuliza maswali na kuwasilisha changamoto zao kwa ajili ya kupata ufumbuzi wa haraka.
“Tupo hapa kwa lengo la kutoa elimu kwa wananchi na kushughulikia kero pamoja na migogoro inayohusiana na masuala ya nishati,” amesema Mniga.

Aidha, amesema ushiriki wa EWURA katika Wiki ya Utumishi wa Umma unalenga kuimarisha uelewa wa wananchi kuhusu haki na wajibu wao katika sekta zinazodhibitiwa na mamlaka hiyo, sambamba na kuendelea kuboresha huduma zinazotolewa kwa jamii.
Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma mwaka huu yameanza Juni 16 na yanatarajiwa kuhitimishwa Juni 25, 2026.

