Na Lucy Ngowi
VIDUKARI ni wadudu wadogo wanaonyonya utomvu wa mimea kupitia majani, mashina au mizizi, hali inayodhoofisha ukuaji wa mazao na kupunguza mavuno.
Wadudu hao pia wana uwezo wa kusambaza magonjwa mbalimbali ya mimea, hivyo kuwa tishio kwa mazao muhimu ya biashara na chakula.
Tanzania kwa sasa inaendelea na jitihada za kisayansi za kukabiliana na wadudu hao wanaojulikana kitaalam kama ‘Yellow sugarcane aphids’
kupitia utafiti unaoongozwa na wataalamu kutoka Idara ya Kilimo na Sayansi ya Ufugaji Nyuki ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) kwa kushirikiana na Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Tanzania (TARI).

Mtafiti kutoka UDSM, Dkt.Wilson Masele, anasema vidukari(Yellow sugarcane aphids) hao katika bara la Afrika waligunduliwa kwa mara ya kwanza nchini Morocco mwaka 2026 kabla ya kuenea katika nchi nyingine ikiwemo Afrika Kusini mwaka 2013, Kenya mwaka 2016 na hatimaye Tanzania mwaka 2020.
Anasema awali wadudu hao walijulikana zaidi kwa kushambulia zao la miwa, lakini watafiti waliona umuhimu wa kuchunguza kama wanaweza pia kuathiri mpunga, ambao ni zao muhimu kwa biashara na usalama wa chakula nchini.
“Miwa ni zao la biashara, lakini mpunga ni zao la biashara na chakula. Ikiwa mdudu huyu ataendelea kuenea na kuathiri mpunga kwa kiwango kikubwa, usalama wa chakula unaweza kuwa hatarini,” anasema.
Kutokana na wasiwasi huo, watafiti walifanya utafiti katika mikoa 17 inayozalisha mpunga kwa wingi na wilaya 34 nchini.
Timu za wataalamu zilifanya uchunguzi mashambani ili kubaini uwepo wa mdudu huyo na kiwango cha athari zake.
Matokeo ya awali yalionesha vidukari hao kuwepo katika baadhi ya maeneo ya mikoa ya Kagera, Morogoro, Kilimanjaro na Manyara.

Watafiti walikusanya sampuli za wadudu hao pamoja na wadudu wengine wanaopatikana katika mazingira ya mashamba ya mpunga ili kuchunguza uhusiano wao na uwezekano wa kutumia maadui wa asili kudhibiti tatizo hilo.
Sambamba na hilo, walikusanya sampuli za mpunga pori na mimea mingine inayopatikana karibu na mashamba ya mpunga ili kubaini kama kuna aina zenye uwezo wa kuhimili mashambulizi ya vidukari hao.
Anasema mradi huo pia umewashirikisha wanafunzi wa shahada za uzamili na uzamivu ambao wanaendesha tafiti mbalimbali.
Anaeleza kuwa, mmoja anachunguza matumizi ya mbinu za kiasili kudhibiti wadudu hao, mwingine anatafuta aina za mpunga zenye uwezo wa kuwa kinzani dhidi ya mashambulizi, huku mwingine akifanya tafiti kuhusu matumizi ya viuatilifu vinavyotokana na mimea.
Kwa maelezo yake, lengo kuu la mradi ni kupata suluhisho la kudumu litakalojumuisha mbegu za mpunga zinazostahimili mashambulizi pamoja na bidhaa salama za kudhibiti wadudu hao.
Kwa mujibu wa watafiti, vidukari hushambulia zaidi wakati wa kuchanua kwa mpunga.
Wadudu hao hufyonza utomvu wa mmea na kuzuia uwezo wake wa kutengeneza chakula, jambo linalosababisha kupungua kwa uzalishaji.
Katika mashambulizi makubwa, hasara inaweza kufikia kati ya asilimia 90 hadi 100 ya mavuno.
Anasena, utafiti pia umebaini kuwa wadudu hao wanaweza kuishi katika mimea mingine.
Kwa mfano, baadhi yao walionekana kwenye zao la bamia mkoani Morogoro pamoja na mimea mingine inayopatikana karibu na mashamba ya mpunga.
Mbali na matokeo ya kisayansi, mradi huo umechangia kukuza rasilimali watu kupitia kuwajengea uwezo watafiti chipukizi na wanafunzi wa vyuo vikuu.
Hii ni sehemu ya utekelezaji wa sera za elimu na ujuzi wa vitendo zinazolenga kuzalisha wataalamu wa ndani wenye uwezo wa kutatua changamoto za taifa.
Mradi huo umefadhiliwa na Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH) kwa zaidi ya Sh. Milioni 300.
Hata hivyo, watafiti wanasema fedha hizo hazikukidhi mahitaji yote ya mradi, hivyo kuna haja ya kuongeza uwekezaji ili tafiti zilizofanyika ziweze kufikia hatua ya kuzalisha bidhaa zinazoweza kutumika na wakulima.
Kwa mtazamo mpana, utafiti huu unaendana moja kwa moja na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inayosisitiza matumizi ya sayansi, teknolojia na ubunifu katika kuongeza uzalishaji wa kilimo, kuimarisha usalama wa chakula, kukuza viwanda vinavyotegemea mazao ya kilimo na kujenga uchumi shindani unaotegemea maarifa.
Kupitia tafiti za aina hiyo, Tanzania inaonyesha uwezo wa kutumia wataalamu wake wa ndani na miundombinu ya kisayansi kutafuta suluhisho la changamoto za kilimo, hatua inayoweka msingi imara wa kufikia maendeleo endelevu na uchumi wa kisasa unaolengwa katika Dira ya 2050.

