Na Lucy Lyatuu,Dodoma
WIZARA ya Elimu, Sayansi na Teknolojia imeiomba Bunge kuidhinisha jumla ya takribani Sh trilioni 2.3 kwa ajili ya kuimarisha sekta ya elimu nchini, ikilenga kuboresha miundombinu, kuongeza ubora wa ufundishaji na kuendeleza matumizi ya teknolojia katika elimu.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda amesema hayo wakati akiwasilisha Bungeni makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara na kwamba fedha hizo zitaelekezwa katika miradi ya kimkakati ikiwemo ujenzi wa madarasa, mabweni, maabara, vyuo vya ufundi pamoja na ununuzi wa vifaa vya kufundishia na kujifunzia.
Amesema kuwa Serikali inaendelea kuipa kipaumbele sekta ya elimu kutokana na mchango wake mkubwa katika kujenga rasilimali watu wenye ujuzi na uwezo wa kuchangia katika uchumi wa taifa.
Aidha, amebainisha kuwa sehemu kubwa ya fedha hizo itaelekezwa kwenye miradi ya maendeleo ili kuhakikisha wanafunzi wote nchini wanapata mazingira bora ya kujifunzia bila changamoto za msingi.
Ameeleza kuwa Serikali imepanga kuongeza ufadhili wa miradi ya utafiti na ubunifu kutoka miradi 80 hadi 109, kwa kuzingatia maeneo ya kipaumbele ya kitaifa. Miradi hiyo inalenga kutatua changamoto mbalimbali ikiwemo mabadiliko ya tabianchi, uchumi wa bluu, uvuvi, maji, kilimo, afya na maendeleo ya viwanda.
Katika hatua nyingine, Serikali kupitia taasisi za elimu ya juu na elimu ya ufundi itatekeleza jumla ya miradi 1,390 ya utafiti katika sekta mbalimbali ikiwemo afya, elimu, biashara, kilimo, uongozi, ushirika, teknolojia, uvuvi, ardhi, mazingira na usanifu majengo. Hatua hii inalenga kuimarisha msingi wa maarifa na ubunifu unaohitajika katika kukuza uchumi wa taifa.
Aidha, Serikali imepanga kuchapisha jumla ya tafiti 2,497 katika majarida ya kitaifa na kimataifa ili kuongeza usambazaji wa maarifa, kuchochea mijadala ya kitaaluma na kuhakikisha matokeo ya utafiti yanatumika katika kutatua changamoto.
Aidha, Serikali imepanga kuchapisha jumla ya tafiti 2,497 katika majarida ya kitaifa na kimataifa ili kuongeza usambazaji wa maarifa, kuchochea mijadala ya kitaaluma na kuhakikisha matokeo ya utafiti yanatumika katika kutatua changamoto za kijamii na kiuchumi.
Katika kuimarisha miundombinu ya utafiti, Serikali itajenga uwezo wa maabara katika taasisi tano za utafiti na maendeleo ili ziwe maabara za rufaa kwa utafiti wa viwanda na ubunifu wa kisasa. Pia, itaimarisha ushirikiano kati ya taasisi za utafiti, elimu ya juu na sekta ya viwanda ili kuongeza mchango wa sayansi katika utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.
Serikali pia itaendelea kuhamasisha wabunifu na kuongeza idadi ya wanufaika wanaopata mikopo kupitia Mfuko wa Ubia na Ubiasharishaji wa Ubunifu wa Samia (Samia Innovation Commercialization Fund). Kupitia mpango huo, vyuo vitano vya Maendeleo ya Wananchi vitapatiwa vituo vya ubunifu ili kuibua na kuendeleza vipaji vya vijana.
Katika kuhakikisha matumizi salama ya teknolojia, Serikali itaimarisha utafiti na udhibiti wa matumizi ya teknolojia ya nyuklia katika sekta mbalimbali. Aidha, itaendelea kukagua vituo 900 vyenye vyanzo vya mionzi na kupima viwango vya mionzi kwa wafanyakazi 2,110 wanaofanya katika mazingira havo ili kulinda afva .