Na Lucy Ngowi
WAZIRI wa Maji, Jumaa Aweso, ametangaza mikakati kabambe ya kuboresha upatikanaji wa maji safi na salama nchini wakati akiwasilisha bajeti ya Wizara kwa mwaka wa fedha 2026/2027 Bungeni, jijini Dodoma.
Amesema Serikali itaendelea kuimarisha huduma ya maji kwa kutumia teknolojia za kisasa, kupanua vyanzo vya fedha na kushirikisha sekta binafsi.

Ili kuongeza kasi ya miradi, Wizara imeanza maandalizi ya Hati Fungani ya Sekta ya Maji itakayovutia uwekezaji kutoka ndani na nje ya nchi.
Aweso amebainisha kuwa Dira 2050 inalenga asilimia 70 ya uwekezaji kutoka sekta binafsi, huku Sera ya Taifa ya Maji ya mwaka 2002 (Toleo la 2025) ikifungua nafasi kwa wadau mbalimbali kushiriki kikamilifu.
Aidha, Mfuko wa Taifa wa Maji utaimarishwa ili kuongeza fedha za miradi na maendeleo ya vyanzo vya maji.
Katika kuboresha huduma, Wizara itaongeza matumizi ya TEHAMA ikiwemo mita za kidijitali (Mita Janja) na maombi ya huduma mtandaoni.
Hadi Aprili 2026, jumla ya mita 23,156 zimefungwa, kutoka 13,526 mwaka 2025, huku lengo likiwa kufunga mita 1,114,133 mijini ifikapo 2030.
Teknolojia hii inalenga kuondoa changamoto za ankara zisizo sahihi na upotevu wa maji.
Aidha, Waziri amesisitiza ushirikiano wa sekta mbalimbali katika matumizi ya rasilimali za maji, ikiwemo ujenzi wa mabwawa ya matumizi ya pamoja na uvunaji wa maji ya mvua.
Kwa mwaka 2026/2027, Wizara imeomba kuidhinishiwa Sh. Trilioni 1.12, ambapo Sh. Bilioni 80.65 ni matumizi ya kawaida na Trilioni 1.03 ni kwa maendeleo.
Mikakati hiyo inalenga kuhakikisha huduma bora na endelevu ya maji kwa wananchi wote.

