Na Mwandishi Wetu
NJOMBE: CHAMA cha Wafanyakazi katika Vyombo vya Habari Tanzania (JOWUTA) kimetaka kuongezwa kwa ushirikishwaji wa vyombo vya habari katika maandalizi na maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani (Mei Mosi) mwaka huu 2026 yatakayofanyika mkoani Njombe.
JOWUTA, ambayo mwaka huu inashiriki kwa mara ya kwanza kama mwanachama wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (TUCTA), imesema pia inatarajia kutoa tuzo kwa wafanyakazi bora katika sekta ya habari.

Akizungumza katika kikao cha maandalizi ya Mei Mosi, mkoani Njombe, Mwenyekiti wa JOWUTA Taifa, Mussa Juma, ameipongeza Kamati ya Habari na Matangazo ya Mei Mosi kitaifa, lakini akabainisha kuwa bado ushiriki wa vyombo vya habari haujaridhisha.
Amesisitiza umuhimu wa kuvishirikisha zaidi vyombo mbalimbali ikiwemo magazeti, redio, televisheni na mitandao ya kijamii katika utoaji wa taarifa na matangazo.
Ameongeza kuwa maudhui ya matangazo yanapaswa kuangazia vivutio na fursa zilizopo mkoani Njombe ili kuutangaza zaidi mkoa huo.
Juma amesema JOWUTA, yenye wanachama zaidi ya 400 nchi nzima, iko tayari kushirikiana na kamati za Mei Mosi kuimarisha utoaji wa taarifa na kuhamasisha ushiriki wa wananchi.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Taifa wa RAAWU, Jane Mihanji, amehimiza umuhimu wa kugharamia magazeti yanayochapisha matoleo maalum ya Mei Mosi, akieleza kuwa yamekuwa yakitoa makala muhimu kuhusu utekelezaji wa miradi ya serikali na sekta binafsi.
Rais wa TUCTA, Tumaini Nyamhokya, amesema maadhimisho hayo ni fursa ya kuitangaza Njombe, akitaja sekta za kilimo cha parachichi, viazi, mbao pamoja na vivutio vya utalii.
Wakati huohuo, Kamati ya maandalizi ya Mei Mosi kitaifa imetembelea ujenzi wa uwanja wa maadhimisho na kuagiza kasi iongezwe ili ukamilike ifikapo Aprili 25 mwaka huu, 2026.

