Na Lucy Ngowi
DODOMA: MBUNGE wa Jimbo la Ngorongoro, Yanick Ndoinyo, ameishauri Serikali kugawa Wilaya ya Ngorongoro na kuboresha miundombinu yake ili kusogeza huduma karibu na wananchi.
Akichangia hotuba ya Waziri Mkuu bungeni Dodoma, amesema ukubwa wa wilaya hiyo unaofikia takribani kilomita za mraba 14,030 unasababisha wananchi kusafiri umbali mrefu, wakati mwingine hadi kilomita 300, kufuata huduma za msingi katika makao makuu ya wilaya.
Amesisitiza haja ya kuanzishwa kwa halmashauri mpya na maeneo mengine ya kiutawala ili kupunguza adha hiyo, akibainisha kuwa huduma kama vitambulisho vya NIDA, vyeti vya kuzaliwa na nyaraka nyingine zinapaswa kupatikana karibu zaidi na wananchi.
Kuhusu miundombinu, Ndoinyo ameeleza kuwa Ngorongoro bado haijaunganishwa na barabara ya lami kuelekea Arusha, hali inayokwamisha maendeleo.
Ametaja umuhimu wa ujenzi wa barabara ya Mto wa Mbu hadi Loliondo, akisema itapunguza muda wa safari kutoka saa 12 hadi chini ya saa tatu.
Katika sekta ya uchumi, amesema wilaya hiyo inategemea ufugaji, kilimo na utalii, huku akihimiza uwekezaji zaidi katika utalii ili kuongeza mapato kwa wananchi.
Pia amesisitiza kuwepo kwa mikakati ya kudumu ya upatikanaji wa malisho ili kulinda mifugo.
Kwa upande wa kilimo, ameeleza kuwa changamoto kubwa ni ukosefu wa masoko na miundombinu ya kuhifadhi mazao, hali inayosababisha hasara kwa wakulima.
Aidha, ameomba Serikali kusitisha kutaifisha mifugo na badala yake kutafuta suluhisho rafiki kwa wafugaji, huku akipongeza juhudi za Rais na Serikali katika kuimarisha maendeleo nchini.

