Na Mwandishi wetu
MOROGORO: JAMII imehamasishwa kushirikiana kushughulikia masuala ya maji na jinsia ili kufungua mlango wa uwezeshaji, usawa, na maendeleo endelevu katika upangaji na utekelezaji wa miradi na sera za Sekta ya Maji.
Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Angellah Kairuki, ametoa wito huo mjini Morogoro wakati wa ufunguzi wa Mdahalo wa Wadau kuhusu Maji na Jinsia, ulioandaliwa na Wizara ya Maji kama sehemu ya maadhimisho ya Wiki ya Maji.
“Bila maji safi na salama, jamii haiwezi kustawi, uchumi hauwezi kukua, na mazingira hayawezi kuendelezwa. Hivyo kila mmoja ana jukumu la kuwa tayari kushirikiana,” amesema Waziri Kairuki.

Waziri huyo pia amesisitiza kuwa Serikali imeweka maji kuwa moja ya vipaumbele muhimu katika jitihada za kuboresha maisha ya wananchi kwa kuweka mikakati na kuimarisha uwekezaji katika sekta hiyo.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji, Mwajuma Waziri, amesema Wizara imejipanga kuhakikisha inatoa majibu ya changamoto zinazowakumba wananchi wa jinsia zote katika upatikanaji wa majisafi na salama.
“Hali hii bado inaathiri makundi mbalimbali, hususan wanawake na wasichana ambao hubeba jukumu kubwa la kutafuta na kusimamia matumizi ya maji katika familia,” amesema.
Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Maji na Mazingira, Jackson Kiswaga, amesema kamati yake ipo tayari kupokea na kuyafanyia kazi mapendekezo ya wadau.
“Kazi kubwa ya Bunge ni kutunga Sheria, kuisimamia Serikali, na kuwawakilisha wananchi. Tunategemea kupitia mdahalo huu kupata mapendekezo ya kuzingatia masuala ya kijinsia ipasavyo,” amesema.
Wiki ya Maji, inayoadhimishwa na Wizara ya Maji kuanzia leo Machi 16 hadi 22, mwaka huu 2026, inalenga kuongeza ufahamu juu ya umuhimu wa maji na kuhimiza ushirikiano wa kijamii katika usimamizi wa rasilimali hiyo muhimu.

