Na Mwandishi Wetu
NAIBU Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Dkt. Ngwaru Maghembe, amefanya mazungumzo na Naibu Waziri wa Uhusiano wa Kimataifa na Ushirikiano wa Afrika Kusini, Thandi Moraka, pembezoni mwa Mkutano wa Baraza la Mawaziri wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) uliofanyika jijini Pretoria Machi 13, 2026.
Mazungumzo hayo pia yalihudhuriwa na Naibu Waziri wa Fedha, Laurent Luswetula, pamoja na Balozi wa Tanzania nchini Afrika Kusini, James Bwana.
Katika mazungumzo yao, viongozi hao walijadili namna bora ya kuimarisha uhusiano na ushirikiano wa kidiplomasia kati ya Tanzania na Afrika Kusini, nchi ambazo zina uhusiano wa kihistoria wa muda mrefu.

Miongoni mwa makubaliano yaliyofikiwa ni kuongeza kasi ya kukamilisha rasimu za hati za makubaliano katika maeneo mbalimbali ili ziweze kusainiwa na kuanza kutekelezwa kwa manufaa ya pande zote mbili.
Aidha, Dkt. Maghembe aliipongeza Afrika Kusini kwa kuwa mwenyeji wa Mkutano wa nchi 20 tajiri zaidi duniani (G20) mwaka 2025, pamoja na maandalizi mazuri ya Mkutano wa Baraza la Mawaziri wa SADC uliofanyika kwa siku mbili, kuanzia Machi 12 hadi 13, 2026, jijini Pretoria.







