Na Lucy Ngowi
DODOMA: WANAWAKE wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi wameungana na wanawake wengine kuadhimisha Siku ya Mwanamke Duniani katika maadhimisho yaliyofanyika wilayani Kongwa, mkoani Dodoma.
Akizungumza baada ya maadhimisho hayo, Kaimu Mwenyekiti wa Wanawake wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali na Afya Tanzania (TUGHE), Joyce Mamkwe, amesema maadhimisho ya mwaka huu 2026 yanaongozwa na kaulimbiu isemayo ‘Haki na usawa kwa wanawake na wasichana, msingi jumuishi wa kufikia Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.’

Amesema kaulimbiu hiyo inalenga kuhimiza ushiriki wa wanawake katika mnyororo mzima wa thamani katika sekta mbalimbali za maendeleo ili kuchochea ustawi wa jamii na taifa kwa ujumla.
Mamkwe ameeleza kuwa wanawake wa wizara hiyo wameshiriki maadhimisho hayo kwa ufadhili wa Mradi wa Kuendeleza Usimamizi wa Uvuvi na Ukuzaji Viumbe Maji wa Bahari Tanzania (TASFAM).
“Leo Wizara ya Mifugo na Uvuvi tupo Kongwa kuadhimisha siku hii muhimu katika maisha ya mwanamke kuanzia anapozaliwa hadi anapokuwa mtu mzima.
“Tunashukuru mradi wa TASFAM ambao umetuwezesha kufika hapa na kujumuika na wanawake wenzetu,” amesema.
Ameongeza kuwa mradi huo una programu ya kuendeleza shughuli za uvuvi na ukuzaji wa viumbe maji katika ukanda wa Pwani, huku wanawake wakitarajiwa kuwa sehemu muhimu ya wanufaika na washiriki wa shughuli hizo.

Kwa upande wake, Teddy Salema kutoka Idara ya Uendelezaji wa Maeneo ya Malisho na Rasilimali za Vyakula vya Mifugo, ameushukuru mradi huo kwa kuwawezesha kushiriki maadhimisho hayo.
Amesema jamii inapaswa kutambua uwezo wa wanawake kwani wakipewa nafasi na kuwezeshwa wanaweza kuchangia maendeleo makubwa ya taifa.
“Wanawake wakipewa nafasi wanafanya mambo makubwa. Hata Rais Samia Suluhu Hassan ameonyesha uwezo mkubwa wa uongozi,” amesema.
Salema ameongeza kuwa wanawake wana mchango mkubwa katika sekta ya mifugo, hususan katika ufugaji, chanjo pamoja na uzalishaji wa malisho na vyakula vya mifugo.

Naye Katibu wa Tawi la TUGHE katika Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Grace Mwaisyelage, amewahimiza wanawake kuendelea kuwaelimisha na kuwawezesha mabinti kwa kuwashirikisha katika shughuli za kiuchumi ili wawe viongozi na wafanyabiashara wakubwa siku zijazo.



