Na Mwandishi Wetu
KIKAO cha Makatibu Wakuu na Maofisa Waandamizi wa Nchi Wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) kimeanza leo, Machi 04 2026, jijini Pretoria, Afrika Kusini, kujadili utekelezaji wa Mpango Mkakati Elekezi wa Maendeleo ya Kikanda (RISDP) wa mwaka 2020-2030.
Ujumbe wa Tanzania unaongozwa na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Said Shaib Mussa, unashiriki kikao hicho cha utangulizi kuelekea Mkutano wa Baraza la Mawaziri wa SADC utakaofanyika Machi 12-13, 2026.
Katika hotuba za ufunguzi, Mwenyekiti wa kikao, Balozi Tebogo Seokolo, na Katibu Mtendaji wa SADC, Elias Magosi, walisisitiza umuhimu wa kutathmini ufanisi wa RISDP na kubaini changamoto zinazokwamisha utekelezaji wake.

Changamoto zilizobainishwa ni pamoja na uhaba wa rasilimali fedha, tofauti kati ya vipaumbele vya kitaifa na kikanda, na kutoridhiana kati ya sera zilizowekwa na utekelezaji halisi wa mpango.
Vilevile, utekelezaji umekabiliwa na madhara ya UVIKO-19, mabadiliko ya tabianchi, changamoto za kiusalama, uhaba wa nishati, uhakika wa chakula, na mabadiliko ya siasa za kimataifa.
Balozi Seokolo amesisitiza kwamba kukabiliana na changamoto hizo kunahitaji mikakati thabiti na utekelezaji wa pamoja ili nchi wanachama ziweze kufanikisha malengo ya RISDP kwa kipindi cha miaka mitano iliyosalia (2026-2030).






