Na Lucy Ngowi
DODOMA: MBUNGE wa Jimbo la Katoro mkoani Geita, Kija Ntemi amehoji Serikali kuhusu upatikanaji wa huduma za Jeshi la Zimamoto na Uokoaji katika jimbo hilo, akitaka ufafanuzi wa lini eneo hilo litapatiwa gari la zimamoto ili kuboresha huduma za dharura.
Ntemi amewasilisha swali hilo bungeni jijini Dodoma, akieleza kuwa ukosefu wa gari la zimamoto umekuwa changamoto kubwa kwa wananchi wa Katoro pindi majanga ya moto na dharura nyingine yanapotokea.
Akijibu swali hilo, Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Ayoub Mohamed Mahmoud, amesema Serikali inaendelea kuchukua hatua madhubuti za kuliimarisha Jeshi la Zimamoto na Uokoaji nchini kama sehemu ya mkakati wa kuimarisha usalama wa wananchi na mali zao.
Amesema Serikali imekuwa ikiipa kipaumbele sekta hiyo kwa kuimarisha vitendea kazi, ikiwemo ununuzi wa magari ya kisasa ya kuzima moto na uokoaji, hatua inayolenga kuongeza uwezo wa jeshi hilo kuwafikia wananchi kwa wakati na kutoa huduma kwa ufanisi.
Naibu Waziri amefafanua kuwa Jimbo la Katoro tayari limepatiwa gari moja jipya la zimamoto na uokoaji aina ya IVECO, ambalo ni la kisasa na linatarajiwa kuboresha kwa kiasi kikubwa utoaji wa huduma za zimamoto katika jimbo hilo na maeneo ya jirani.
Aliongeza kuwa kwa sasa gari hilo lipo mkoani Dar es Salaam likikamilishiwa taratibu za mwisho kabla ya kusafirishwa kwenda mkoani Geita.
Kwa mujibu wa ratiba, gari hilo linatarajiwa kuwasili Geita Februari 9, 2026.
Naibu Waziri alisema ujio wa gari hilo utaimarisha usalama wa wananchi wa Katoro kwa kusaidia kukabiliana kwa haraka na majanga ya moto pamoja na dharura nyingine, hivyo kupunguza athari zinazoweza kujitokeza.

