Na Lucy Lyatuu
TAASISI ya Utafiti wa Misitu Tanzania (TAFORI) imewasisitiza Watanzania kuchangamkia fursa zilizopo katika sekta ya Misitu na Nyuki, kuwekeza katika misitu na kushiriki katika ufugaji nyuki kwa kuzingatia njia sahihi zilizofanyiwa utafiti ili kupata tija katika rasilimali hizo
Wito huo umetolewa na Mkurugenzi wa Utafiti wa Matumizi ya Misitu Dkt. Chelestino Balama wakati akizungumza na baadhi ya timu ya wataalamu wa misitu na nyuki na Waandishi wa Habari waliofika ofisi za TAFORI Mkoani Morogoro, kutembelea baadhi ya tafiti zinazofanywa.
“Sisi kama taasisi ya TAFORI tunafanya tafiti ambazo ni kwa ajili ya kuboresha vipato kwa jamii lakini pia kwa ajili ya kuboresha uchumi wa nchi yetu .
“Mojawapo ni tafiti ya kuzalisha miti katika maeneo mbalimbali ili kuwa na taarifa sahihi za miti anbayo inafaa kupandwa katika eneo fulani ambapo Vijana wengi wamejikita huko na imekuwa ni sehemu ya ajira.
“Lakini pia taasisi yetu imefanya utafiti ambao unahusika na kuangalia rasilimali za misitu ikiwemo kuona ni namna gani zinachangia kwenye kuokoa malighafi katika viwanda vya Misitu hapa nchini na utafiti huu umekuwa na mchango mkubwa kwenye kuleta ajira kwa vijana, maana wamejikita kuanzia kwenye mnyororo mzima. wa Mazao ya misitu”.
Ofisa Mtafiti Mkuu kutoka TAFORI ambaye pia ni Kaimu Mkurugenzi tafiti ya uzalishaji Misitu Dkt. Stephen Maduka ameeleza
uwepo wa bustani ya miti ya Utafiti ya TAFORI kwa lengo la kunusuru miti ya asili isitoweke.
Miti hiyo ni Mkurungu, Msandali na Msekeseke inayovunwa kwa wingi kwa ajili ya biashara ya utengenezaji samani, kuongeza thamani ya miti ya asili ya matunda.
Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi wa Utafiti wa Ufugaji Nyuki TAFORI Allen Kazimoto amewataka Vijana na Wanawake kushiriki kikamilifu katika Ufugaji Nyuki kwa kuzingatia ubora wa Mazao ya Nyuki yanayokudhi soko la ndani na pia la Kimataifa ili waweze kupata tija katika Ufugaji.