Na Mwandishi Wetu
MFUKO wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF) umeshiriki katika mjadala wa kitaaluma ulioandaliwa na Chama cha Waajiri Tanzania (ATE), uliobeba mada isemayo, “Kuimarisha Hifadhi ya Jamii na Uendelevu wa Biashara kupitia Ushirikiano wa Kimkakati, Ufanisi wa Mifumo ya Udhibiti na Ushirikiano wa Taasisi.”
Mjadala huo umefanyika Juni 25, 2026 jijini Dar es Salaam, wakati wa Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Waajiri ulioambatana na Kongamano la Waajiri, ukijumuisha wadau mbalimbali kutoka sekta ya ajira, hifadhi ya jamii na taasisi nyingine muhimu.
Akichangia katika mjadala huo, Mkuu wa Kitengo cha Takwimu na Hadhari wa WCF, James Tenga, ameelezea umuhimu wa kuimarisha mifumo ya hifadhi ya jamii kwa kuweka nguvu kwenye matumizi ya teknolojia na miradi ya kimkakati kama Jamiinamba.

Aidha, amebainisha kuwa, tukiweza kushirikiana na kutumia mifumo hii vizuri, itasaidia kupanua wigo wa wanachama, kuongeza fursa za ajira, na kuleta tija pamoja na ukuaji wa kiuchumi kwa mifuko ya hifadhi, waajiri na wafanyakazi kwa ujumla.
Ushiriki wa WCF katika kongamano hilo umeendelea kuimarisha ushirikiano kati ya taasisi za hifadhi ya jamii, waajiri na wadau wengine muhimu, kwa lengo la kukuza mazingira bora ya kazi, kuimarisha ulinzi wa wafanyakazi, na kuhakikisha uendelevu wa shughuli rasmi za biashara nchini.


