Na Lucy Ngowi
DODOMA: MBUNGE wa Bukoba Vijijini, Dkt. Jasson Rweikiza, ameuliza katika kipindi cha maswali na majibu Bungeni mjini Dodoma: “Je, lini wananchi wa Bukoba watawezeshwa kwa kupewa vizimba vingi zaidi vya samaki ili kushiriki katika kukuza uchumi?”
Akijibu swali hilo, Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Ng’wasi Kamani amesema kuwa Serikali kupitia Wizara yake, kwa kushirikiana na Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB), inaendelea na zoezi la utoaji wa mikopo ya masharti nafuu kwa ajili ya vizimba, vifaranga na chakula cha samaki.
Amesena katika awamu ya kwanza, mikopo ya vizimba 44 ikijumuisha vizimba 30 Bukoba, 12 Muleba na viwili Misenyi yenye thamani ya Sh. 986.80 milioni ilitolewa mkoani Kagera kwa wanufaika 101.
Alisema zaidi kwamba katika mwaka wa fedha 2025/2026, Wizara imepokea kiasi cha Sh. bilioni 7 kutoka Hazina kwa ajili ya kuwezesha vijana kupata mitaji kupitia mikopo yenye masharti nafuu.
Amesema fedha hizo zitatumika kukopesha vijana 308 waliohitimu mafunzo, wakiwemo vijana 32 kutoka Mkoa wa Kagera.
Aidha, Wizara inatarajia kupokea sehemu ya Sh. bilioni 200 ambazo ni ahadi ya Rais Samia Suluhu Hassan ndani ya siku 100, zitakazoelekezwa katika kuwezesha mikopo ya vizimba.
Wizara pia inaendelea kutafuta vyanzo vingine vya fedha ili kuendelea kutoa mikopo ya vizimba katika maeneo mbalimbali nchini ikiwa ni pamoja na kwa vijana wa Bukoba.
Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Kamani, ameongeza kwamba Serikali inahimiza Halmashauri kutenga asilimia 10 ya mikopo yao kwa shughuli za ufugaji samaki iwapo kuna maeneo yanayofaa kwa shughuli hiyo, ili kuongeza uwekezaji wa vizimba na fursa za ajira kwa wananchi.

