Na Lucy Ngowi
PWANI: KATIBU Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Carolyne Nombo amesema viongozi bora hujenga mazingira wezeshi kwa wahadhiri na watafiti kustawi , kupanda vyeo kwa haki bila mizengwe na kukuza ushirikiano wa kimataifa kwa manufaa ya taifa.
Profesa Nombo amesema hayo alipokuwa akihitimisha Warsha ya Mafundo na Tafakuri kwa Viongozi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), iliyofanyika Katika Shule ya Uongozi ya Mwalimu Julius Nyerere iliyopo Kibaha mkoani Pwani,

Pia amewataka viongozi wa Vyuo Vikuu nchini kuendelea kuwa nguzo ya mabadiliko chanya kwa kukuza mazingira ya ubunifu, utafiti wenye tija na maendeleo ya kitaaluma yanayozingatia haki na uwazi.
“Uongozi wa vyuo vikuu unapaswa kuwa chachu ya ubunifu, utafiti wenye tija na machapisho ya kitaaluma yanayochangia maendeleo ya jamii,” amesema.
Amewapongeza viongozi wapya walioteuliwa na kuwatakia kila la heri katika majukumu waliyopewa

Pia kwa wale wanaoendelea na uongozi amewataka kuendeleza mafanikio waliyofikia na kuacha alama ya uongozi bora katika taasisi hiyo,
“Mungu awabariki muongoze vyema , awape hekima na uvumilivu katika utekelezaji wa majukumu yenu,” amesema.
Naye Makamu Mkuu wa UDSM, Profesa William Anangisye amesema kuandaa warsha kama hiyo kunahitaji rasilimali watu na fedha hivyo ametambua mchango wa wadhamini wote waliofanikisha shughuli hiyo.

Amesema elimu waliyoipata kwenye mafundo hayo iwe chachu ya kuendeleza misingi ya utawala bora, ubunifu na mwelekeo wa kimkakatikatika kuifikisha taasisi yao katika dira yake ya mwaka 2061.
” Basi sote hatuna budi kuwa mabalozi wa mabadiliko chanya kwenye maeneoyetu ya kazi,” amesema.