Na Lucy Ngowi
DAR ES SALAAM: SERIKALI imesisitiza dhamira yake ya kuendelea kuwawezesha vijana wanaoanzisha na kuendeleza biashara kwa lengo la kuongeza ajira, kukuza viwanda na kuimarisha uchumi wa taifa.
Waziri wa Viwanda na Biashara, Judith Kapinga, amesema Serikali ya Awamu ya Sita imefanya maboresho mbalimbali ya kisera, kisheria na kiutawala yaliyoboresha mazingira ya biashara na uwekezaji, ikiwemo kupunguza urasimu, kuondoa baadhi ya tozo na kuimarisha huduma za kidijitali.

Akizungumza katika uzinduzi wa kinywaji cha KIX jijini Dar es Salaam, Kapinga amesema vijana wanaochangamkia fursa za uwekezaji wanapaswa kuungwa mkono, akimtaja mwanzilishi wa bidhaa hiyo kuwa mfano wa kuigwa kwa kuwekeza nchini.
Amesema sekta binafsi ina mchango mkubwa katika uchumi wa taifa kwa kuzalisha ajira nyingi, huku serikali ikiendelea kuweka mazingira rafiki yatakayochochea ukuaji wa viwanda, biashara, kilimo na uchumi wa kidijitali.
Aidha, ameipongeza kampuni ya Amount Group Limited kwa uamuzi wake wa kuwekeza Tanzania na kueleza kuwa mpango wa kujenga kiwanda cha uzalishaji wa KIX unaonesha imani kubwa kwa mazingira ya biashara yaliyopo nchini.

Kapinga pia amewahimiza wafanyabiashara kuzingatia sheria, viwango vya ubora, utunzaji wa mazingira na uwajibikaji kwa jamii ili kujenga biashara endelevu, huku akiwataka Watanzania kuunga mkono bidhaa zinazozalishwa nchini kwa kuwa ushindani huongeza ubora, ajira na mapato ya taifa.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Amount Group Limited, Justine Ishengerema, amesema kampuni hiyo inalenga kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha uzalishaji na usambazaji wa kinywaji cha KIX katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kati kupitia ujenzi wa kiwanda kikubwa cha kisasa.

