Na Mwandishi Wetu
NAIBU Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, Amina Khamis Shabaan, amesema kuwa ushirikiano kati ya Tanzania na Africa50 utafanikisha miradi ya kimkakati na kuimarisha ushirikiano katika ya miundombinu.
Amina amebainisha hayo nchini Marekani, alipokutana na kufanya mazungumzo na Mkurugenzi Mkuu, anayesimamia Mikakati, Uhusiano na Uwekezaji wa Africa50, Jon-Pierre Fourie, Kando ya Mikutano ya Mwaka ya Benki ya Dunia na Shirika la Fedha la Kimataifa, IMF.

Pamoja na mambo mengine, wamejadiliana namna ya kuwa na ushirikiano endelevu Kupitia ubunifu, uwekezaji na ujenzi wa uwezo wa ndani ya Bara la Afrika.
Aidha, Serikali ilipongeza dira ya Africa50 ya kuendeleza miradi ya kijani (green infrastructure) inayoendana na Mpango wa Tatu wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka Mitano (FYDP III) na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Serikali ilithibitisha dhamira yake ya kuendeleza ushirikiano huo, ikisisitiza kwamba kupitia ubia na Africa50, Afrika inaweza kujenga miradi yenye mabadiliko makubwa katika viwanda, biashara za kikanda na kuboresha maisha ya wananchi utakaoleta matokeo halisi ya maendeleo kwa Bara la Afrika.
