Na Mwandishi Wetu
WAZIRI wa Fedha, Balozi Khamis Mussa Omar, amesema Sh. Bilioni 883.93, sawa na Dola za Marekani milioni 351.04, zimetumika katika kutekeleza miradi mbalimbali ya maji na usafi wa mazingira nchini.
Akizungumza wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa Mapitio ya Pamoja wa Sekta ya Maji, ulioandaliwa na Wizara ya Maji mjini Morogoro, Balozi Khamis amesema fedha hizo zilipatikana kutoka kwa wadau wa maendeleo na vyanzo vya ndani vya serikali.
Mkutano huo ni sehemu ya maandalizi kuelekea Siku ya Maji Duniani, itakayoadhimishwa Machi 22, mwaka huu 2026.

Balozi Khamis pia ameipongeza Sekta ya Maji kwa mafanikio makubwa yaliyopatikana katika utekelezaji wa miaka 20 ya Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Maji (WSDP).
Amesema tangu kuzinduliwa mwaka 2006, huduma ya maji mjini imeongezeka kutoka asilimia 74 hadi 92.5, na vijijini kutoka asilimia 54 hadi 85.2.
Aidha, alibainisha kuwa mkutano huo ni jukwaa la ngazi ya juu la majadiliano na tathmini ya utekelezaji wa WSDP, huku akisisitiza umuhimu wa wadau kushirikiana katika kuhakikisha upatikanaji wa maji unaendelea kuboreshwa.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji, Mwajuma Waziri, amesema Serikali ya Awamu ya Sita imejipanga kuhakikisha upatikanaji wa maji nchini unafikia asilimia 100.
“Hadi sasa, vijiji 10,758 tayari vimeshapata huduma ya maji ya uhakika, huku vijiji 1,575 bado vikiwa nyuma,” amesema.
Amesisitiza kuwa miradi mikubwa ikiwemo Mpango wa Gridi ya Taifa ya Maji inaendelea kutekelezwa ili kufikia malengo hayo.
Mwajuma ameongeza kuwa mkutano huo ni fursa ya wadau kushirikiana, kuchambua mafanikio na changamoto zilizojitokeza, na kupanga mikakati ya utekelezaji wa WSDP awamu ya tatu kwa kipindi cha Januari hadi Desemba 2025.
Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Kigoma Malima, amemshukuru Waziri wa Maji, Jumaa Aweso, na watendaji wa wizara kwa kufanya maadhimisho ya Wiki ya Maji Mkoani Morogoro.
Amesema mkoa wa Morogoro ni mdau muhimu wa sekta ya maji na unatambua jukumu lake la kuhifadhi vyanzo vya maji, kwani ni chanzo kikuu cha maji kwa mikoa ya Dar es Salaam na Pwani.

