SERIKALI imesema inaendelea kutekeleza mikakati mbalimbali ya kukuza Sekta ya Maliasili na Utalii ili kuongeza mchango wake katika uchumi wa taifa, ajira na mapato ya ndani.
Akizungumza Bungeni mjini Dodoma wakati wa uwasilishaji wa hotuba ya Mapato na Mwelekeo wa Kazi za Serikali kwa mwaka wa fedha 2026/2027, Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba amesema hatua hizo tayari zimeanza kuleta matokeo chanya.
Kwa mujibu wa Waziri Mkuu, idadi ya watalii waliotembelea hifadhi za taifa imeongezeka kwa asilimia 10.73, kutoka watalii 5,360,247 mwaka 2024 hadi kufikia 5,935,561 mwaka 2025.

Aidha, mapato yatokanayo na utalii yameongezeka kutoka dola za Marekani Bilioni 3.9 mwaka 2024 hadi kufikia Bilioni 4.4 kufikia Desemba 2025, sawa na ongezeko la asilimia 12.82.

Katika kikao hicho cha tatu cha Bunge la 13, kilichohudhuriwa pia na Waziri wa Maliasili na Utalii Dkt. Ashatu Kijaji, Waziri Mkuu alieleza kuwa mafanikio hayo yanachangiwa na juhudi za Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kukuza sekta hiyo.
Kutokana na mchango huo, Januari 31, 2026, Rais Samia alitunukiwa tuzo ya Kiongozi Mwenye Maono katika hafla ya Serengeti Awards.
Anaripoti Mwandishi Wetu

