Na Lucy Ngowi
DODOMA: SERIKALI imeendelea kuchukua hatua madhubuti kuhakikisha wahitimu wa vyuo wanapata fursa za ajira kupitia utekelezaji wa miradi ya kimkakati, uendelezaji wa viwanda vidogo na vya kati pamoja na programu za ubunifu nchini.
Hayo yameelezwa na Naibu Waziri wa Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano ya Kazi, Rahma Kisuo, leo Januari 30, 2026, Bungeni jijini Dodoma, wakati akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Dkt. Regina Malima aliyehoji mikakati ya Serikali katika kuongeza ajira kwa wahitimu wa vyuo.
Kisuo amesema kupitia miradi ya kimkakati, Serikali imefanikiwa kuzalisha ajira nyingi ikiwemo zaidi ya ajira 35,000 zilizotokana na ujenzi wa Reli ya Kisasa (SGR), pamoja na zaidi ya ajira 10,000 kutoka katika mradi wa ujenzi wa Bomba la Mafuta Ghafi la Afrika Mashariki (EACOP).

Ameongeza kuwa miradi mingine iliyochangia upatikanaji wa ajira ni pamoja na ujenzi wa Bwawa la Kuzalisha Umeme la Mwalimu Julius Nyerere uliotoa zaidi ya ajira 10,000 na ujenzi wa Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Msalato jijini Dodoma uliotoa zaidi ya ajira 1,500,
Pia ujenzi wa Daraja la JPM (Kigongo–Busisi) uliotoa zaidi ya ajira 1,500, pamoja na upanuzi wa Bandari ya Dar es Salaam uliotoa zaidi ya ajira 3,000.
Akijibu swali hilo, Naibu Waziri amesema Serikali pia imetoa mafunzo ya uzoefu wa kazi kwa wahitimu 29,902 wa ngazi mbalimbali za elimu, sambamba na kutoa mafunzo ya kuongeza ujuzi kwa wafanyakazi 19,075 katika sekta za hoteli, madini, usafirishaji, kilimo na usindikaji wa mazao ya kilimo kupitia Programu ya Taifa ya Kukuza Ujuzi.
Aidha, ameongeza kuwa Serikali imeandaa Mwongozo wa Taifa wa Mafunzo kwa Vitendo kwa Wahitimu unaolenga kuweka utaratibu wa utoaji wa mafunzo ya uzoefu wa kazi kwa wahitimu.
Mwongozo huo unatumika kwa waajiri wote katika sekta ya umma na binafsi ili kuhakikisha wahitimu wanapata ujuzi unaoendana na mahitaji ya soko la ajira.

