Na Mwandishi Wetu
DODOMA: SERIKALI imetangaza mpango wa kujenga barabara ya Kakonko–Muhanga kupitia Gwarama yenye urefu wa kilomita 41.43 kwa kiwango cha lami, hatua inayolenga kurahisisha usafiri na usafirishaji kwa wananchi na wafanyabiashara.
Hayo yamebainishwa leo Aprili 8, 2026, Bungeni jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Ujenzi, Godfrey Kasekenya, wakati akijibu swali la Mbunge wa Kakonko, Alan Mvano (CCM), aliyetaka kufahamu ni lini barabara hiyo itajengwa kwa kiwango cha lami.
Kasekenya amesema barabara hiyo ni barabara kuu inayosimamiwa na Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS), Mkoa wa Kigoma, na kwa sasa Serikali ipo katika hatua za awali za kuandaa upembuzi yakinifu pamoja na usanifu wa kina.
Hii ni hatua muhimu kabla ya kuanza ujenzi rasmi wa lami.
Aidha, ameongeza kuwa mara usanifu utakapokamilika na gharama halisi za ujenzi zikajulikana, Serikali itahakikisha fedha za utekelezaji zinapatikana ili kuanza ujenzi.
Katika hatua nyingine, Naibu Waziri Kasekenya amemuagiza Meneja wa TANROADS Mkoa wa Kigoma kuhakikisha barabara hiyo inakaguliwa na kufanyiwa matengenezo ya muda ili iweze kupitika kikamilifu, hivyo wananchi kupata huduma bora za usafiri na usafirishaji wakati ikisubiri ujenzi wa lami.

