Na Lucy Ngowi
DODOMA: RAIS wa Chama cha Walimu Tanzania (CWT), Dkt. Suleiman Ikomba, amewaonya walimu na watumishi wa chama hicho kuacha tabia ya uchonganishi na kueneza taarifa zisizo na msingi, akisema mwenendo huo unadhoofisha utendaji na mshikamano ndani ya taasisi.
Dkt. Ikomba ametoa onyo hilo alipokuwa akizungumza na Kamati ya Utendaji ya Taifa ya CWT pamoja na watumishi wa Makao Makuu ya chama katika kikao kilichofanyika St. Gaspar, jijini Dodoma.
Amesema CWT ina dhamana kubwa kwa walimu wa Tanzania, hivyo mafanikio yake hayategemei viongozi waliochaguliwa pekee, bali pia juhudi, uadilifu na ushirikiano wa watumishi wake.
Amekiri kuwepo kwa changamoto za kiutumishi katika Makao Makuu ya chama, zikiwemo migogoro, kutokuelewana, kupungua kwa ushirikiano baina ya idara na tabia ya uchonganishi, hali inayosababisha baadhi ya watumishi kufanya kazi kwa mashaka.
“Ni lazima tukubaliane kuwa mazingira ya aina hii hayawezi kusaidia taasisi kusonga mbele kwa ufanisi tunaoutarajia,” amesema.
Amesisitiza umuhimu wa kuheshimu majukumu na mamlaka ya kila nafasi ndani ya chama, akieleza kuwa ingawa viongozi huchaguliwa kwa vipindi maalum, taasisi yenyewe ni ya kudumu na inahitaji utamaduni wa kuheshimiana.
Aidha, amewataka watumishi kufanya kazi kwa misingi ya taaluma, uadilifu na kuepuka upendeleo, huku akionya kuwa kujihusisha na makundi au kampeni za uchaguzi wa ndani huacha athari hasi katika utendaji baada ya uchaguzi.
“Tunachohitaji ni utamaduni wa kuweka mbele maslahi ya chama na wanachama wake badala ya makundi au maslahi binafsi,” amesisitiza.
Ameeleza matarajio ya uongozi kuwa kila idara itekeleze majukumu yake kwa kuzingatia mipango kazi, kuimarisha ushirikiano miongoni mwa watumishi, na kuheshimu taratibu za kiutumishi.
Dkt. Ikomba amesema ana imani kuwa watumishi wanaweza kurekebisha hali iliyopo na kujenga upya mazingira bora ya kazi, akisisitiza kuwa Makao Makuu yanapaswa kuwa mfano wa nidhamu, weledi na mshikamano kwa wanachama kote nchini.
Amewataka watumishi kuanza ukurasa mpya kwa kufanya kazi kwa pamoja, kuheshimiana na kuweka mbele maslahi ya chama, akibainisha kuwa taasisi yoyote inayotaka kufanikiwa lazima ijengwe juu ya misingi ya nidhamu, uwajibikaji na uadilifu.
Ameongeza kuwa uongozi utaendelea kusimamia kwa karibu utendaji wa kazi ili kuhakikisha kila mtumishi anatimiza wajibu wake ipasavyo.
“Ni matumaini yangu kuwa tutafanya kazi kwa mshikamano na kuweka mbele maslahi ya chama. Tukisimama pamoja, CWT itaendelea kuwa imara na yenye heshima kwa walimu na taifa kwa ujumla,” amesema.

