a Lucy Lyatuu, Dodoma
MAMLAKA ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali (GCLA), imesema zaidi ya Sh bilioni 32.25 zimetumika kununua mitambo 32 mikubwa pamoja na vifaa saidizi 542, jambo ambalo limeongeza ufanisi na ubora wa uchunguzi wa sampuli mbalimbali.
Aidha imesema katika mwaka mmoja kuanzia February 2025/2026 imefanywa uchunguzi wa sampuli na vielelezo mbalimbali vipatavyo 247,286 jambo linaloongeza uelewa wa hali ya juu kwa jamii.
Mkemia Mkuu wa Serikali, Dk. Fidelice Mafumiko amesema hayo wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu kutangaza miradi ya maendeleo na fursa za vijana kwa mwaka 2025/2026, alisema uwekezaji huo umesaidia kutoa huduma bora zaidi kwa wananchi.
Kadhalika amesema kuanzia February 2025/2026 imetengeneza ajira zaidi ya 145,000 zikiwemo za vijana wakishiriki katika suala zima la kemikali kwenye uingizwaii, usafirishaji pamoja na uhifadhi.
Amesema MAMLAKA imeongeza na kuimarisha uwekezaji mkubwa katika mitambo na vifaa vya kisayansi ili kuimarisha huduma za uchunguzi wa maabara nchini.
Amesema uchunguzi unaofanywa na maabara hiyo umechangia Kwa kiwango kikubwa Kwa jamii, kupunguza athari za dawa za kulevya kwa vijana, kuthibitisha ubora na usalama wa bidhaa za dawa asili zinazozalishwa na wataalamu wakiwemo vijana, na kutoa fursa za ajira na kujiajiri.
Aidha, ameongeza kuwa maabara hiyo inasaidia kutatua changamoto za kijamii kama kuthibitisha uhalali wa wazazi kwa watoto, kutatua migogoro ya mirathi kupitia vipimo vya DNA, na kusaidia huduma za matibabu kama kusafishwa na kupandikizwa figo, pamoja na utambuzi wa sumu kabla na baada ya kifo.
Dk. Mafumiko pia ameongeza kuwa wajasiriamali vijana wanatumia maabara hizo kupima ubora wa bidhaa zao kabla ya kuziuza sokoni, huku vyuo vikuu vinapata punguzo la asilimia 75 ya gharama za uchunguzi kwa ajili ya tafiti za kisayansi.
Aidha amesema licha ya mafanikio lakini MAMLAKA inakabiliwa na changamoto ikiwemo utegemezi wa wataalamu kutoka nje ya nchi katika matengenezo ya mitambo, jambo linaloongeza gharama. Ili kukabiliana na hili, Mamlaka inaendelea kuwajengea uwezo watumishi wake kufanya matengenezo hayo wenyewe.

