Na Mwandishi Wetu
ARUSHA: WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu- Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu, Ridhiwani Kikwete amesema moja ya changamoto kubwa kwa sasa ni ufahamu hafifu wa kuwepo kwa fedha maalum zinazotengwa toka kwenye manunuzi ya Umma.

Ridhiwani amesema hayo alipozungumza katika Kongamano lililoandaliwa na Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA), lililolenga kujadili Ununuzi wa umma na Ukuzaji wa kampuni za wazawa na makundi maalum kwa ukuaji wa Uchumi Jumuishi katika zama za mabadiliko ya teknolojia ama Kidigitali lililofanyika Jijini Arusha Juni 16, 2025.
Amesema jambo muhimu ni kutoa elimu na kuwashirikisha wadau wakiwemo madiwani na wakurugenzi wa Halmashauri, Manispaa na Majiji ili elimu ya kuwepo kwa fedha maalum zinazotengwa toka kwenye manunuzi ya Umma ijulikane.

“Umuhimu na msisitizo kama huu umesaidia sana vijana, wanawake na wenye ulemavu kukimbilia zile asilimia 10 zinazotengwa na Halmashauri kutoka kwenye mapato ya ndani,”amesema.
Pia ameeleza umuhimu wa kuendelea kutambua kuwa mabadiliko mbalimbali yaliyofanywa na serikali yanalengwa kuwasaidia na kukuza ustawi wa Watu wenye mahitaji maalum.
Amesema serikali imewezesha vijana na watu wenye ulemavu waweze kujiinua kiuchumi ikiwemo maelekezo ya kisheria ya kuendelea kutenga Asilimia 30 ya zabuni za ununuzi wa umma.

Ridhiwani pia amewashukuru PPRA kwa kazi nzuri na kutambua umuhimu wa kuandaa kongamano hilo ambalo kwa hakika linalenga kuwawezesha wananchi.