Na Lucy Ngowi
DODOMA: WAZIRI wa Maji, Jumaa Aweso, amesema Wizara ya Maji inaendelea na mpango wa ufungaji wa dira za maji za malipo kabla ya matumizi kwa wateja binafsi, taasisi na biashara, hatua inayolenga kumaliza kero ya ubambikizaji wa ankara za maji kwa wananchi.
Akizungumza na waandishi wa habari leo Januari 28, 2026, kuhusu utekelezaji wa ahadi za Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika siku 100 za uongozi wake baada ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025,

Waziri Aweso amesema changamoto ya malalamiko ya ankara za maji imekuwa kubwa, hivyo wizara imechukua mikakati ya kuboresha huduma kwa wateja wapya mijini na vijijini.
Amesema hadi sasa wizara imenunua dira za maji za malipo kabla 2,271 ambazo zinaendelea kufungwa katika maeneo mbalimbali nchini, akisisitiza kuwa maunganisho ya maji kwa mteja mpya hayapaswi kuzidi siku saba.
Aidha, ameitaka sekta ya maji kuimarisha matumizi ya mifumo ya kidijitali katika maeneo yote ya utoaji huduma.
Katika hatua nyingine, Waziri Aweso amesema ujenzi wa mabwawa ya ukubwa wa kati ya Gidahababieg, Mwambazi na Mwamashindike unaendelea kwa kasi, yakitarajiwa kuhifadhi zaidi ya mita za ujazo 1,457,000 za maji na kunufaisha wananchi zaidi ya 1,817,800 pamoja na mifugo 356,400.

Pia amesema serikali imeimarisha uhifadhi wa vyanzo vya maji kwa kupanda miti zaidi ya 705,300, kugawa pikipiki 216 kwa Jumuiya za Watoa Huduma za Maji Ngazi ya Jamii (CBWSOs), kulipa Sh. Bilioni 198.84 kwa wakandarasi, kuchimba visima 151 na kulipa fidia kwa wananchi waliopisha miradi ya maji.
Hatua hizo, amesema, zinaonesha dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita ya kuhakikisha huduma ya maji safi, salama na endelevu kwa wananchi.

