Na Danson Kaijage
DODOMA: Taasisi ya Tiba ya Mifupa Muhimbili (MOI) imewafuata wananchi huko waliko kupitia huduma za kliniki tembezi, njia inayoleta urahisi wa huduma za afya.
Daktari Bingwa wa upasuaji wa mifupa kutoka MOI, Tumaini Minja amesema hayo wakati wa Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea jijini Dodoma.
Amesema kupitia ushiriki wao kwenye maonesho hayo, MOI imefanikiwa kuhudumia zaidi ya wananchi 70 waliojitokeza kupatiwa huduma za uchunguzi na ushauri wa kitaalamu, hasa kwa magonjwa ya mifupa, nyonga, magoti na mgongo.
“Tumekutana na wananchi wengi waliokuwa wakihitaji huduma maalum ambazo kwa kawaida hupatikana Dar es Salaam pekee.
“Kupitia kliniki hii tembezi, tumewafikia wananchi wa Dodoma na mikoa ya jirani kwa urahisi zaidi, na bado tutaendelea kuwafikia wananchi wengi zaidi lengo ni kuona wa Tanzania wananufaika na huduma za matibabu kwa urahisi na ufanisi,” amesema.
Amesema lengo la taasisi hiyo, ni kuhakikisha huduma bora za afya ya ubongo, mgongo, mishipa ya fahamu na mifupa zinawafikia Watanzania wote kwa usawa.
“Tunaendelea kutoa huduma hata baada ya maonesho kumalizika, na tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais Samia na Serikali kwa kutuwezesha kufanya haya kupitia kliniki tembezi inayojumuisha madaktari bingwa mbalimbali,” amesema.
Pia taasisi hiyo inatoa elimu ya afya kwa wananchi ili kusaidia jamii kutambua mapema dalili za maradhi sugu yanayohusiana na mifupa na mgongo, hivyo kupunguza athari zinazoweza kujitokeza kwa kuchelewa kutafuta tiba.
Amesema huduma hizo za karibu na wananchi zitakuwa endelevu, wametoa wito kwa wananchi kuchangamkia fursa kila timu ya madaktari bingwa inapokuwa katika mikoa yao.
“Tumekutana na wananchi wengi waliokuwa wakihitaji huduma maalum ambazo kwa kawaida hupatikana Dar es Salaam pekee,” amesema.