Na Lucy Ngowi
NAIROBI – KENYA — WAANDISHI wa Habari kutoka Afrika wamekutana jijini Nairobi kwa ajili ya mafunzo kuhusu mbinu za kuandika habari za uhamiaji
Mafunzo hayo ya siku tatu yameandaliwa chini ya Mpango wa Pamoja wa Uhamiaji wa Wafanyakazi (JLMP) kwa ushirikiano na Tume ya Umoja wa Afrika, IOM, ILO na Shirikisho la Waandishi wa Habari Afrika (FAJ), yakilenga kuwajengea uwezo waandishi wa habari kuandika habari za uhamiaji kwa mtazamo wa Kiafrika na kwa kuzingatia ukweli.

Akifungua mafunzo hayo, Mkuu wa Kanda ya Afrika Mashariki Edwin Righa, amesesitiza umuhimu wa nafasi ya waandishi wa habari katika kuifanya mitazamo ya umma kuhusu uhamiaji.
“Ninyi ni watafuta ukweli, waandaaji wa ajenda na wanasimulia hadithi kwa niaba ya jamii. Nafasi yenu ni ya kipekee katika jinsi ya kuripoti uhamiaji unaeleweka na kuzungumzwa katika jamii zetu,” amesema.
Amesena Bara la Afrika linapitia mabadiliko makubwa ya kiuchumi, huku vijana wengi wakihamia kutoka nchi moja hadi nyingine kutafuta ajira, heshima na maisha bora.
Amesema kuwa maelezo mengii kuhusu uhamiaji yanayotawala vyombo vya habari si ya kina na mara nyingi hujikita kwenye siasa au hofu kuliko uhalisia.
“Mara nyingi tunasimulia zaidi habari za majanga. Ingawa si vibaya, tunapaswa pia kuangazia mchango wa maendeleo unaotokana na uhamiaji,” amesena.

Righa amewataka waandishi kutumia takwimu kuandika habari zilizo bora, za haraka na za kuaminika, zitakazosaidia umma kupata taarifa sahihi zinazotegemewa.
“Mafunzo haya pia yanajengwa juu ya msingi wa Mtandao wa Waandishi wa Habari wa Uhamiaji wa Wafanyakazi wa Afrika, uliozinduliwa mwaka 2023 kwa lengo la kukuza uandishi wa habari wa kimaadili na wa ushirikiano barani Afrika.
“Ushiriki wenu unaonesha namna maono haya yanavyoimarika — kuwakutanisha waandishi na watunga sera, na kusogeza zaidi simulizi za uhamiaji kwenye maisha halisi ya wahusika,” amesema.
Katibu Mkuu wa Chama cha Waandishi wa Habari Kenya (KUJ), Erick Oduor ameeleza kusikitishwa kwake na hali ya habari nyingi za uhamiaji barani Afrika kuandikwa na vyombo vya habari vya kimataifa.

“Mafunzo haya yanatufundisha namna ya kurudisha simulizi hizi mikononi mwa Waafrika na kuandika habari zinazotokana na hali halisi ya bara letu,” amesema.
Oduor ameeleza kuundwa kwa mtandao wa kikanda wenye wawakilishi saba kutoka nchi mbalimbali za Afrika Mashariki, zikiwemo Kenya, Uganda, Rwanda, Tanzania, Sudan Kusini, Seychelles na Comoro.
Kwa lengo la kusukuma ajenda ya uandishi wa habari za uhamiaji katika kila nchi kwa kuzingatia ukweli na takwimu sahihi.
Akitoa mfano, Oduor ameeleza jinsi chama chao kilivyofanikiwa kujumuisha kipengele katika makubaliano ya kazi na shirika moja la habari la kimataifa jijini Nairobi ili kuwalinda wafanyakazi wahamiaji.
“Tunapaswa kufikiria pia kuhusu wale wanaofanya kazi katika nchi zetu bila kuwa raia wa nchi husika. Hawa pia wanahitaji haki na ulinzi kazini,” amesena.

Oduor amesisitiza umuhimu wa vyombo vya habari kushirikishwa tangu mwanzo wa mijadala ya sera za uhamiaji.
“Tusiwakumbuke waandishi wa habari tu kunapokuwa na janga. Vyombo vya habari ni washirika muhimu katika uundaji wa sera,” amesema.
Mafunzo hayo yataendelea kwa siku mbili zaidi, yakiwa na matarajio ya kuzalisha simulizi mpya na mtandao thabiti wa waandishi ambao wataweza kubadilisha taswira ya uhamiaji barani Afrika — kwa usahihi, kwa uhalisia na kwa athari chanya kwa jamii.