Na Mwandishi Wetu, Dodoma
DODOMA: Mkoa wa Dodoma umeanza kuvunja dhana ya kuwa ni eneo linalofaa kwa mazao machache kutokana na ukame, baada ya jaribio la kwanza la viazi mviringo lililofanywa na Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Tanzania (TARI) kuonesha mafanikio makubwa.
Jaribio hilo lililofanyika katika shamba la Makamu wa Rais Mstaafu, Dkt. Philip Mpango, Kijiji cha Mayamaya, Wilaya ya Bahi, limedumu siku 104 hadi hatua ya uvunaji na kuthibitisha kuwa zao hilo linaweza kustawi katika mazingira ya Dodoma, likifungua fursa mpya ya chakula, biashara na kuongeza kipato kwa wakulima.
Mafanikio hayo yamekuja wakati wakulima wa Dodoma wakitakiwa kupanua wigo wa mazao badala ya kutegemea mazao machache, huku utafiti na teknolojia za kilimo zikitajwa kuwa njia ya kukabiliana na changamoto za ukame na kuongeza uzalishaji.
Akizungumza baada ya kuvuna viazi hivyo, Dkt. Mpango aliwataka wakazi wa Dodoma kuanza kujiandaa kuchangamkia fursa hiyo mara utafiti utakapokamilika na mbegu hiyo kuanza kutolewa rasmi.
“Wakazi wa Dodoma sasa tuanze kuchangamkia hii fursa na TARI wako tayari kutusaidia kwa kutupatia mbegu bora zinazofaa zaidi. Hii itatusaidia chakula na kipato kwa ajili ya kusaidia watoto wetu kwenda shule,” alisema.
Alisema mafanikio hayo yanaonesha kuwa Dodoma si lazima itegemee mtama, mahindi, zabibu au alizeti pekee, bali inaweza kuongeza mazao mengine kupitia maarifa ya kilimo na matumizi sahihi ya maji.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa TARI, Dkt. Thomas Bwana, alisema taasisi hiyo inapanga kuendeleza majaribio ya zao hilo kwa wakulima wadogo wanaotegemea mvua, hatua itakayosaidia kutathmini uwezo wa zao hilo katika maeneo mbalimbali.
Alisema TARI itaendelea kufanya tafiti katika maeneo tofauti nchini ili kuondoa dhana kwamba eneo fulani linafaa kwa zao moja pekee, huku akiwataka wakulima kuruhusu taasisi hiyo kufanya majaribio ya teknolojia na mbegu katika mashamba yao.
Mtafiti Kiongozi wa zao hilo kutoka TARI Uyole, Dkt. Owekisha Kwigizila, alisema mbegu hiyo mpya inaweza kukomaa ndani ya takribani siku 90, kustahimili ukame na baadhi ya magonjwa, huku ikiwa na uwezo wa kuzalisha tani 35 hadi 40 kwa hekta moja.
Wakazi wa Mayamaya walioshiriki katika uvunaji huo walisema wamevutiwa na namna zao hilo lilivyostawi katika eneo hilo na kuonesha utayari wa kuanza kulima endapo utafiti utakamilika na mbegu kupatikana.

