Na Lucy Ngowi
DODOMA: MAMLAKA ya Afya ya Mimea na Viuatilifu Tanzania (TPHPA) imeanza mpango wa kupanua uchunguzi wa visumbufu vya mazao katika maeneo mbalimbali nchini, kwa lengo la kutengeneza ramani ya kitaifa itakayoonyesha mtawanyiko wa visumbufu na kuwawezesha wakulima kutumia viuatilifu sahihi kwa wakati na katika maeneo husika.
Hatua hiyo inalenga kubadili mfumo wa udhibiti wa visumbufu kutoka matumizi ya viuatilifu kwa mazoea kwenda kwenye udhibiti unaotegemea taarifa sahihi za kisayansi, hatua inayotarajiwa kupunguza gharama za uzalishaji, hasara za mazao na matumizi yasiyo sahihi ya viuatilifu.
Akizungumza katika Maonesho ya Nanenane, Profesa Joseph Ndunguru kutoka TPHPA, amesema mamlaka imeanza kupata taarifa muhimu kupitia teknolojia inayowezesha kubaini visumbufu vya mazao, ikiwemo bakteria, virusi, fangasi na wadudu, hata pale ambako dalili zake haziwezi kuonekana kwa macho.
Amesema ramani hiyo itakapokamilika, itawezesha wataalamu na wakulima kufahamu aina za visumbufu vinavyopatikana katika maeneo mbalimbali na kupanga hatua za udhibiti kulingana na tatizo lililopo.
“Ukipeleka kiuatilifu sahihi katika eneo sahihi na kudhibiti kisumbufu sahihi, tunapata udhibiti endelevu wa visumbufu,” amesema.
Amesema uchunguzi uliofanyika katika Halmashauri ya Wilaya ya Mpwapwa umeonyesha umuhimu wa teknolojia hiyo, baada ya kubaini visumbufu mbalimbali katika mazao ya mihogo, vitunguu, karanga, Chinese cabbage na sukuma wiki.
Kwa mujibu wa Profesa Ndunguru, katika mihogo zilibainika changamoto zinazohusisha utitiri, bakteria na fangasi, wakati vitunguu vilibainika kuwa na visumbufu vinane, vikiwemo bakteria na fangasi.
Amesema katika karanga vilibainika visumbufu vitatu, ikiwemo kirusi kinachoweza kusababisha majani kuwa ya njano na mimea kudumaa, huku Chinese cabbage ikiwa na visumbufu sita na sukuma wiki ikibainika kuwa na bakteria, fangasi na virusi.
Amesema taarifa hizo zitasaidia TPHPA na wataalamu wa kilimo kutoa mapendekezo sahihi ya udhibiti kwa kuzingatia aina ya kisumbufu na eneo kinapopatikana, badala ya wakulima kutumia dawa kwa kubahatisha.
Naye Ofisa Kilimo wa Halmashauri ya Mpwapwa, Salum Ally, amesema teknolojia hiyo imewasaidia wataalamu kubaini changamoto ambazo haziwezi kuonekana kwa macho na kutoa ushauri unaoendana na tatizo halisi la mazao.
Ameomba uchunguzi huo kupanuliwa katika maeneo mengi zaidi nchini ili wakulima wanufaike na taarifa sahihi kuhusu visumbufu na namna bora ya kuvidhibiti.

