Mkurugenzi wa Kurugenzi ya Tafiti na Uchumi Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Dkt. Suleiman Misango (kulia), akizungumza mbele ya Kaimu Mkurugenzi wa Uendeshaji Mfuko wa PSSSF,, Hajj Moshi.
Na Mwandishi Wetu
DODOMA: MKURUGENZI wa Tafiti na Uchumi wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Dkt. Suleiman Misango, amepongeza mfumo wa kidijitali wa PSSSF Portal baada ya kushuhudia jinsi unavyowezesha taarifa za wanachama kupatikana kwa haraka, akisema ni hatua kubwa ya kuboresha utoaji wa huduma za hifadhi ya jamii.
Dkt. Misango ametoa pongezi hizo, baada ya kuhudumiwa katika banda la Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) kwenye Maonesho ya Nanenane yanayoendelea katika Viwanja vya Dkt. John Malecela, Nzuguni, jijini Dodoma.
Amesema alishangazwa na kasi ya mfumo huo baada ya kutaja jina lake na kuona taarifa zake zote za uanachama, kuanzia alipoanza ajira hadi sasa, zikionekana mara moja.
“Mimi ni mwanachama wa PSSSF wa muda mrefu, lakini nilipotaja tu jina langu, taarifa zangu zote zikaonekana mara moja. Hii inaonesha mfumo umeboresha sana utoaji wa huduma,” amesema.

Mkurugenzi wa Kurugenzi ya Tafiti na Uchumi Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Dkt. Suleiman Misango (katikati), akizungumza mbele ya Kaimu Mkurugenzi wa Uendeshaji wa Mfuko wa PSSSF, Hajj Moshi (kushoto) na Meneja Mawasiliano wa BoT, Vicky Msina, kwenye Maonesho ya Nanenane Viwanja vya Dkt. John Malecela jijini Dodoma Agosti nne, 2026
Ameongeza kuwa tofauti na ilivyokuwa zamani, ambapo watumishi walilazimika kutafuta mafaili kwa muda mrefu, sasa taarifa zinapatikana kwa kubonyeza kitufe kimoja, hatua inayorahisisha upatikanaji wa huduma popote kupitia PSSSF Portal.
Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi wa Uendeshaji wa PSSSF, Hajj Moshi, amesema Mfuko unaendelea kuhamasisha wanachama kutumia PSSSF Portal ili wajihudumie kwa urahisi popote na wakati wowote.
Amesema matumizi ya mfumo huo yameongeza ufanisi wa huduma na kusaidia utekelezaji wa kampeni ya “Tunalipa Jana”, inayowezeshwa na utunzaji bora wa kumbukumbu, matumizi ya teknolojia ya kidijitali na uwezo wa kifedha wa Mfuko.
Aidha, amesema maonesho hayo yanatoa fursa ya kuwafikia wanachama, kuwapatia elimu kuhusu huduma za kidijitali na kuwaunganisha na mfumo wa PSSSF Portal, ambao umeendelea kukidhi mahitaji ya wanachama, hususan vijana wanaopendelea huduma za kidijitali.
Katika ziara hiyo, Moshi ametembelea mabanda mbalimbali, yakiwemo ya Taasisi za Elimu ya Juu, Ofisi ya Rais na Ofisi ya Waziri Mkuu (TAMISEMI), ambapo alizungumza na wanachama na kupokea maoni yao kuhusu huduma zinazotolewa na Mfuko.

