Na Lucy Ngowi
DAR ES SALAAM: WAZIRI wa Viwanda na Biashara, Judith Kapinga, amesema Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba) yatakayofanyika kuanzia Juni 28 hadi Julai 13, 2026, yatakuwa ya kipekee kutokana na kuadhimisha Jubilei ya Miaka 50 tangu kuanzishwa kwake.
Akizungumza na waandishi wa habari, Kapinga amesema maonesho hayo yameendelea kuwa jukwaa muhimu la kukuza biashara, uwekezaji, ubunifu na ushirikiano wa kiuchumi kati ya Tanzania na mataifa mbalimbali.
Kaulimbiu ya mwaka huu 2026 ni “Maonesho ya Biashara ya Kimataifa Sabasaba: Bidhaa za Tanzania, Masoko ya Kimataifa,” inayolenga kuhamasisha wazalishaji wa ndani kupanua masoko ya bidhaa zao.
Amesema zaidi ya waoneshaji 3,000 kutoka mataifa zaidi ya 23 wanatarajiwa kushiriki, huku wageni zaidi ya 500,000 wakitarajiwa kutembelea maonesho hayo, ambayo pia yatazalisha maelfu ya ajira za moja kwa moja na zisizo za moja kwa moja.
Kapinga amesema Serikali imekamilisha maboresho katika Viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere, ikiwemo mabanda ya maonesho, huduma za maji na umeme, pamoja na matumizi ya teknolojia ya kidijitali. Mfumo wa kuwaongoza wageni kwenye mabanda na programu ya Biashara App utarahisisha ununuzi wa tiketi kwa njia ya mtandao na kupunguza foleni.
Ameongeza kuwa wananchi watapata fursa ya kuona teknolojia mpya, bidhaa za viwandani, ubunifu wa vijana na fursa za biashara na uwekezaji, sambamba na burudani na michezo ya watoto.
Amewakaribisha wafanyabiashara, wawekezaji, wajasiriamali na wananchi kushiriki maonesho hayo ya kihistoria na kunufaika na fursa mbalimbali za biashara na teknolojia.

