Na Lucy Lyatuu, Dodoma
TUME ya Taifa ya Umwagiliaji (NIRC) imesema katika kutekeleza programu ya uchimbaji wa visima kwa ajili ya shughuli za umwagiliaji, hadi sasa imechimba visima 362 katika mikoa minne juhudi hizo zikilenga kuongeza uhakika wa uzalishaji wa mazao kwa wakulima wadogo nchini.
Imetaja mikoa ambayo hadi sasa imefikiwa kwa uchimbaji huo kuwa ni pamoja na Geita, Tabora, Manyara na Singida.
Mkurugenzi Msaidizi wa Eneo la Utafiti anayesimamia programu ya uchimbaji wa visima, Naomi Mcharo, amesema hayo wakati akizungumza na katika banda la tume hiyo kwenye Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea katika Viwanja vya Chinangali Park jijini Dodoma,.
Amesema Serikali imeanzisha huduma hiyo kufuatia maelekezo ya Rais Samia Suluhu Hassan yaliyolenga kuwasaidia wakulima kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi kupitia kilimo cha umwagiliaji chenye uhakika.
Amesema visima hivyo vimekuwa vikilenga zaidi kuwafikia wakulima wadogo, ambapo kisima kimoja kimekuwa na uwezo wa kuhudumia takribani hekari 40 zinazolimwa na wakulima wasiopungua 16 wenye mashamba ya kati ya hekari mbili hadi mbili na nusu kila mmoja.
“Mpaka sasa tumeshachimba visima 362 na mashine zetu ambazo Serikali ilitusaidia kuzinunua zinaendelea na kazi katika mikoa ya Mara, Njombe na Mtwara. Lengo letu ni kuhakikisha programu hii inawafikia wakulima wengi zaidi nchini,” amesema Mcharo.
Ameongeza kuwa tume imekuwa ikishirikiana na halmashauri za wilaya kutambua na kuhakiki vikundi vya wakulima vinavyonufaika na programu hiyo, huku kila wilaya ikianza na visima vitano katika hatua ya kwanza. Aidha, amesema wakulima binafsi wenye mashamba ya kuanzia hekari 20 hadi 40 wanaweza kuwasilisha maombi kwa tume ili kuchimbiwa visima kwa utaratibu maalumu unaojumuisha ruzuku ya asilimia 20 ya gharama za uchimbaji.

Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma mwaka 2026 yameanza Juni 16 katika Viwanja vya Chinangali Park jijini Dodoma na yanatarajiwa kuhitimishwa Juni 23, huku taasisi mbalimbali za umma zikiendelea kutoa elimu na kuhamasisha wananchi kuhusu huduma wanazozitoa.
Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Taifa ya Umwagiliaji na Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu, Maria Itembe, amesema wananchi wamekuwa wakijitokeza kwa wingi kupata taarifa kuhusu huduma za umwagiliaji zinazotolewa na taasisi hiyo.
Amesema tume hiyo imeendelea kusimamia ujenzi wa miundombinu mipya ya umwagiliaji, ukarabati wa miundombinu ya zamani, ujenzi wa mabwawa pamoja na uchimbaji wa visima katika maeneo yenye ukame ili kuongeza upatikanaji wa maji kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji.

