Na Mwandishi Wetu
DAR ES SALAAM: SERIKALI imewahimiza vijana nchini kuchangamkia Programu ya Mama Samia ya Utambuzi na Urasimishaji wa Ujuzi inayotekelezwa hadi Juni 2027, ikilenga kutambua, kuthibitisha na kurasimisha ujuzi walioupata kupitia uzoefu wa kazi, mafunzo kazini na njia nyingine zisizo rasmi za kujifunza.
Akizungumza katika Mahafali ya 18 ya Chuo cha Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi Furahika kilichopo Buguruni Malapa, Wilaya ya Ilala jijini Dar es Salaam, Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Wanu Hafidh Ameir, amesema Serikali itaendelea kuimarisha elimu ya ujuzi na umahiri ili kuwajengea vijana uwezo wa kujiajiri na kushindana katika soko la ajira.

Amesema programu hiyo inalenga kuwafikia vijana 80,000 nchini na kuwapa fursa ya kutambulika rasmi kwa ujuzi walionao, hata kama hawakupitia mfumo rasmi wa elimu.
“Kupitia programu hii hakuna ujuzi unaopotea kwa kukosa utambuzi rasmi. Niwasihi vijana wote wenye ujuzi walioupata nje ya mfumo rasmi kujitokeza na kutumia fursa hii kurasimisha ujuzi wao,” amesema Wanu.
Ameongeza kuwa Serikali inaendelea kuunganisha mafunzo yanayotolewa vyuoni na mahitaji halisi ya soko la ajira kwa kuimarisha ushirikiano kati ya taasisi za elimu, sekta binafsi na viwanda, hatua inayolenga kuongeza umahiri unaohitajika katika mazingira ya kazi.
Wanu pia amepongeza Chuo cha VETA Furahika kwa mchango wake katika kuwawezesha vijana kupata stadi za kazi, pamoja na Mbunge wa Jimbo la Ukonga, Bakari Shingo, kwa kusaidia vijana wengi kupata mafunzo ya ufundi.
“Nimeelezwa kuwa Mhe. Shingo amefadhili wanafunzi 220, baadhi yao wakihitimu leo. Haya ni mafanikio makubwa yanayotokana na ushirikiano mzuri kati ya Serikali na wadau wa maendeleo,” amesema.
Aidha, amewataka wahitimu kutumia elimu na ujuzi walioupata kujenga ajira na fursa za maendeleo, huku akisisitiza umuhimu wa nidhamu, ubunifu, uzalendo na ujasiriamali katika kufanikisha ndoto zao na kuchangia ukuaji wa uchumi wa taifa.
Kwa upande wake, Mbunge wa Ukonga, Bakari Shingo, amesema amefadhili wanafunzi 220 katika chuo hicho kwa kutumia utaratibu wa kutangaza fursa kupitia gari la matangazo ili kuwafikia vijana wengi zaidi wanaohitaji mafunzo ya ufundi.
Naye Mkuu wa Chuo hicho, Dkt. David Cleopa Msuya, amesema chuo kina wanafunzi 460 na kinatoa kozi mbalimbali za ufundi zikiwemo Usimamizi wa Hoteli, Kompyuta, Umeme, Urembo, Ushonaji, Utalii pamoja na Uondoshaji Mizigo Bandarini.

