Na Lucy Ngowi
KUTOKANA na changamoto ya gharama kubwa ya chakula cha mifugo nchini, watafiti wa Kitanzania wamebuni chakula maalumu cha kuku wa nyama kinacholenga kupunguza gharama za ufugaji huku kikiongeza uzalishaji na ubora wa kuku.
Mtafiti na mbunifu wa mradi huo, Dkt. Whitefrank Frank, anasema ubunifu huo umetokana na tafiti za muda mrefu zilizolenga kutafuta suluhisho la changamoto zinazowakabili wafugaji wengi wa kuku nchini, hasa gharama kubwa za chakula, dawa na uzalishaji.
Dkt. Frank anasema alianza kushiriki katika shughuli za Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia Tanzania (COSTECH) tangu mwaka 2018 kupitia programu za ubunifu za MAKISATU chini ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia.

Kwamba, nwaka 2022 walipata mtaji wa awali wa dola za Marekani 5,700 kwa ajili ya kuhakiki wazo lao na kuligeuza kuwa biashara.
Anaeleza kuwa, kupitia kampuni yao ya Afrimix Animal Feeds inayojihusisha na shughuli za kilimo na mifugo, walifanya tafiti kuhusu mahitaji ya wafugaji wa kuku wa kisasa na wa kienyeji.
Watafiti hao walibaini kuwa changamoto kubwa ipo katika ubora na gharama ya chakula cha kuku.
“Tuliona kuna ombwe kubwa sokoni, hivyo tukaanza kufanya tafiti maabara kabla ya kwenda sokoni.
“Tumeunda fomula ya chakula cha kuku wa nyama inayotumia malighafi zinazopatikana kwenye mazingira yetu kama mimea, wadudu na mahindi,” anasema.
Anasema chakula hicho kina uwezo wa kuongeza uzito wa kuku kwa muda mfupi huku kikisaidia kuku kujenga kinga ya mwili ya asili, jambo linalopunguza matumizi ya dawa na gharama kwa mfugaji.
Kwa kushirikiana na wataalamu kutoka Chuo Kikuu cha Kilimo cha Sokoine ( SUA), walifanya majaribio kwa vifaranga karibu 800 na kubaini kuwa kuku waliolishwa chakula hicho waliweza kufikia uzito wa kilo 1.5 hadi 2 ndani ya muda mfupi.
Aidha, anasema matumizi ya chakula hicho yanaweza kupunguza muda wa ufugaji kutoka wiki nne hadi tatu, hali ambayo itawaongezea wafugaji faida kutokana na mzunguko mkubwa wa biashara.

Kwa sasa bidhaa hiyo bado haijaanza kuuzwa rasmi sokoni, lakini wapo katika hatua za mwisho za maandalizi ya uzalishaji kwa kushirikiana na Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia Tanzania (COSTECH).
Dkt. Frank anasema soko la chakula cha kuku nchini bado lina uhitaji mkubwa kwani takribani asilimia 60 ya mahitaji ya chakula hicho bado hayajafikiwa.
Kutokana na hali hiyo, wamepanga kuanza usambazaji katika mikoa ya Dar es Salaam, Pwani na Morogoro kabla ya kupanua biashara kwenda Dodoma, Singida, Kilimanjaro na Arusha.
Anaeleza kuwa changamoto nyingine inayowakabili wafugaji wengi ni kutofuata kanuni bora za ufugaji pamoja na ukosefu wa elimu sahihi kuhusu lishe ya kuku.
“Wafugaji wengi wameaminishwa kuwa kuku lazima walishwe aina fulani ya chakula pekee, wakati jambo muhimu ni kufuata kanuni bora za ufugaji na kumpa kuku lishe sahihi yenye virutubisho,” anasema.
Anaongeza kuwa serikali kupitia Mamlaka ya Maabara ya Mifugo Tanzania (TVLA) imeweka miongozo ya utengenezaji wa chakula cha mifugo ili kuhakikisha usalama na ubora wa bidhaa hizo.
Mbunifu huyo anasema wanahitaji uwekezaji zaidi kutoka sekta binafsi ili kusaidia kuongeza uzalishaji na kuwafikia wafugaji wengi zaidi nchini.
Kwa mujibu wa Dkt. Frank, mradi huo unaendana na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inayosisitiza matumizi ya sayansi, teknolojia na ubunifu katika kukuza uchumi wa viwanda, kuongeza ajira na kuimarisha usalama wa chakula nchini.
Anasema utafiti huo pia unachangia kuongeza upatikanaji wa protini kwa Watanzania kupitia ufugaji wa kuku wa nyama, huku ukiwawezesha wafugaji wadogo na wa kati kuongeza kipato chao kupitia teknolojia nafuu na endelevu.
“Tunataka kujenga kampuni yenye utamaduni wa kufanya biashara kwa kutegemea tafiti na ubunifu. Tunaamini hatua hii itasaidia kufikia malengo ya maendeleo ya taifa ifikapo mwaka 2050,” anasema.

