Na Lucy Ngowi
MBUNGE wa Buhigwe mkoani Kigoma, Profesa Pius Yanda, ameishauri Serikali kupitia Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kuongeza bajeti ya tafiti katika vyuo vikuu ili kuviwezesha taasisi hizo kutoa mchango mkubwa zaidi katika maendeleo ya taifa.
Profesa Yanda ametoa ushauri huo bungeni alipokuwa akichangia makadirio ya mapato na matumizi ya wizara hiyo kwa mwaka wa fedha 2026/2027, akisema uwekezaji wa kutosha katika utafiti utaviwezesha vyuo vikuu kushindana kimataifa na kuzalisha maarifa yenye tija kwa jamii.
Amesema kwa miaka iliyopita vyuo vikuu vilikuwa vikisaidiwa na serikali pamoja na washirika wa maendeleo katika shughuli za utafiti, lakini bado kuna haja ya kuweka mkakati thabiti wa kuhakikisha eneo hilo linaimarishwa zaidi.
Aidha, Profesa Yanda ameeleza kuwa ongezeko la wanafunzi katika ngazi mbalimbali limeongeza mzigo kwa wahadhiri, hali inayopunguza muda wa kufanya tafiti.
Amempongeza Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kutoa fedha za kuajiri wahadhiri wapya, hatua inayosaidia kupunguza changamoto ya upungufu wa watumishi vyuoni.
Hata hivyo, amesisitiza umuhimu wa kuzingatia miongozo ya Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU) katika ajira hizo, akibainisha kuwa uwiano wa wahadhiri wakongwe na vijana ni muhimu katika kuimarisha ubora wa elimu na utafiti.
Profesa Yanda amesema vyuo vikuu havipaswi kujikita katika ufundishaji pekee, bali pia kufanya tafiti zitakazosaidia maendeleo ya kijamii na kiuchumi.
Ameongeza kuwa ameshiriki katika maandalizi ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 kupitia timu ya wataalamu waliokuwa wakichakata taarifa na kutoa mapendekezo ya kitaalamu.
Pia ameshauri Tanzania kuiga mifumo ya baadhi ya nchi za Afrika zinazotumia wataalamu kuchambua taarifa za maendeleo kila baada ya miaka mitano ili kuboresha mipango ya maendeleo ya taifa.

