Na Mwandishi Wetu
DODOMA: ASKOFU wa Kanisa la Anglikana, Dayosisi ya Central Tanganyika, Dkt. Dickson Chilongani, ameitoa wito kwa Serikali kushughulikia kero mbalimbali zinazowakabili Watanzania ili kudumisha amani, haki na ustawi wa jamii.
Akizungumza leo jijini Dodoma wakati wa ibada ya maadhimisho ya sikukuu ya kumbukizi ya kufufuka kwa Yesu Kristo, iliyofanyika katika Kanisa Kuu la Roho Mtakatifu, Dkt. Chilongani amesema kuwa hatua zaidi zinahitajika ili kutatua changamoto zinazowakwamisha wananchi katika maisha yao ya kila siku.
Amesema kuwa, licha ya juhudi zilizofanywa na Serikali ikiwemo kuongeza mishahara kwa watumishi wa umma mwaka jana, bado kuna matatizo mengi yanayohitaji kushughulikiwa, hususan katika utoaji wa huduma serikalini.
“Tunashukuru kwa jitihada zilizofanyika, lakini bado kuna kero nyingi katika ofisi mbalimbali ambazo zinapaswa kupatiwa ufumbuzi wa haraka,” amesema.
Askofu Chilongani ametaja baadhi ya kero hizo kuwa ni pamoja na urasimu usio wa lazima, vitendo vya kunyimwa haki na ongezeko la rushwa, ambavyo vinaathiri utoaji wa huduma na haki kwa wananchi.
Ameongeza kuwa baadhi ya watumishi wamekuwa wakidai kile kinachoitwa ‘uwezeshwaji’, hali ambayo kimsingi ni rushwa, na kwamba vitendo hivyo vinafanyika waziwazi bila aibu.
“Unapotuma mtu kufuatilia jambo muhimu, anakwambia anaombwa ‘facilitation’. Hili ni tatizo kubwa, na wakati mwingine hata taasisi za dini zinaombwa kutoa fedha hizo. Serikali inapaswa kuingilia kati hali hii,” amesisitiza.
Katika kuhitimisha mahubiri yake, Dkt. Chilongani ameipongeza nchi kwa kuendelea kuwa na amani, umoja na mshikamano, akisisitiza umuhimu wa kuilinda misingi hiyo.
Amefananisha hali hiyo na simulizi ya wanawake waliokwenda kaburini kwa Yesu, ambapo waliondolewa hofu na changamoto zao na kubadilishiwa furaha, akieleza kuwa ni wajibu wa Serikali kuhakikisha Watanzania wanaishi kwa furaha kwa kuondoa kero zinazowakabili.

